Mahakama yaagiza IPOA kumchunguza OCS wa Embakasi kuhusiana na madai ya ukatili

Mahakama ya Makadara imeagiza mamlaka huru ya shughuli za polisi (IPOA) kumchunguza afisa anayesimamia kituo cha polisi cha Embakasi kuhusiana na madai ya ukatili.

Agizo hilo linatokana na madai ya mshukiwa Jefferns Kitemi Kiema kwamba OCS, Moses Wanyama na maafisa wengine walimchapa na kutishia kumuua.

“Mwili wangu wote wauma. Nilichapwa kama mbwa, na sasa wamewasilisha mashtaka feki dhidi yangu. Waliniambia hakuna mahali nitawapeleka na sitakuwa wa kwanza kuauwa,” Kiema aliambia mahakama.

Kiema aliambia hakimu mkuu Angelo Kithinji huku akitoa nguo kuonyesha vidonda mwilimi mwake kwenye mgongo na shingo.

Ameshtakiwa kwa kuharibu fimbo ya mamlaka ya OSC mnamo Septemba 12, eneo la Pipeline Embakasi.

Pia anashtumiwa kwa kuzuia afisa wa polisi kutekeleza majukumu yake.

Stakabadhi za mahakama zaonyesha kwamba kisa hicho kilitokea siku ya Jumamosi mwendo wa saa nne unusu usiku wakati maafisa wa polisi walikuwa wakitekeleza kanuni za kafyu.

Katika eneo la Pipeline kulingana na stakabadhi za korti, maafisa hao walipata gari lililokuwa limeegeshwa katikati mwa barabara na hivyo kuzuia lori lao kupita.

Maafisa wanne kisha walishuka kutaka kujua nini kilikuwa kinaendelea. Kiema anasemekana kutoka nje ya gari hilo akiwa mlevi na mwenye kiburi.

OCS alijiunga na maafisa hao kumhoji mshukiwa. Hapo ndipo anasemekana kuchukuwa fimbo ya mamlaka ya OCS na kuivunja.

Kiema alikanusha mashtaka hayo lakini alikiri kuwa nje wakati wa kafyu.

Alisema alikuwa akihisi uchungu na kwamba hajapelekwa kupokea matibabu tangu alipokamatwa.

Hakimu aliambia Ipoa kufanya uchunguzi na kuwasilisha ripoti mahakamani Septemba 28. Kiema aliachiliwa kwa dhamana ya shilingi elfu tano.