Mama mkwe Kanifinyia jicho..nifanye nini?

kilonzo
kilonzo
Yamewafanyikia wengi ambao wameshindwa hata kuyaeleza. Lakini Japhet  Kilonzo anasema hawezi tena kunyamazia  kitu ambacho kimekuwa kikimfanyikia kila wakati mama wa mke wake anapowatembelea au wanapokutana .

Kilonzo anasema katika jamii yake, mama mkwe ni mtu wa heshima sana na kuna vitu ambavyo hafai hata kuvifanya.  Baada ya kuwa na mke wake  kwa miaka mitano alitaraji kwamba mama mkwe ataweza kuwacha waishi maisha yao bila usumbufu wake.

Lakini unajiuliza ni usumbufu upi  huu? Mama mkwe wake Kilonzo amekuwa akimkonyezea jicho ! Kilonzo haelewi mbona lakini anasema wakati mmoja mkewe hakuwa nyumbani na mama mkwe ndiye aliyekuwa ameachwa na watoto. Miongoni mwa majukumu yake siku hiyo ilikuwa kuwatayarishia watoto chakula cha mchana  lakini mama mtu aliamua kuitumia fursa hiyo kujaribu kufanya kitendo kisichoweza kutarajiwa kutoka kwa mama mkwe.

‘Aliponiletea chakula, alinipa maji ya kunawa mikono kisha akanikaribia akitaka kunikalia miguuni. Nilishtushwa na kitendo hicho na kumskuma kando. Nilishangaa nini kimemwingia lakini hiyo haikuwa mwisho wa majaribio yake’ anasema Kilonzo. Wanapozungumza mama mkwe humuambia vitu vingine kwa mafumbo  kuashiria kwamba  anachomfanyia mwanawe naye mama mkwe anaweza kukifanya hata bora zaidi.

Kilonzo ameogopa kumuambia mkewe kuhusu tabia za mamake na hilo limemsumbua kwa muda  sana. Hataki kuharibu uhusiano kati ya mkewe na mamake na pia kwa sababu wajukuu zake wanampenda sana na mgogoro wowote utakaozuka utawatenganisha na nyanya yao.

Kila  wakati mama mkwe anapomuangalia, yeye humfinyia jicho hatua ambayo anasema inavuruga heshima ambayo inafaa kuwepo kati ya mtu na mama mkwe wake . Kilonzo yupo katika njia panda, je amuambie mke wake kuhusu tabia za mamake au anyamaze na aendelee kupitia  masaibu haya? Ungefanya nini iwapo ungejipata katika hali hii ya Kilonzo?