Seneta Irungu Kang'ata, mbunge wa Maragua Mary Wamaua, Wangari Mwaniki wa Kigumo na mbunge wa Gatanga Nduati Ngugi walikutana na PK katika hoteli ya Greens huko Thika.
Wakati wa mkutano huo wa saa tatu waliahidi kushirikiana na Kenneth kuendeleza ajenda ya rais na kuliunganisha eneo la Mlima Kenya kabla ya uchaguzi mkuu ujao.
Kenneth amekuwa akipigiwa upato kwa uwezekano wa kujiunga na baraza la mawaziri na hata kutajwa kuwa miongoni mwa wanoweza kumrithi rais Uhuru Kenyatta katika eneo la Mlima Kenya.
Wiki jana, Kenneth alikuwa katika mkutano mwingine uliowaleta pamoja spika wa bunge Justin Muturi, waziri wa kilimo Peter Munya, magavana Kiraitu Murungi (Meru), Ndiritu Muriithi (Laikipia), na kiongozi wa wengi bungeni Amos Kimunya katika dhifa ya chakula cha mchana kwenye hoteli ya Panafric Hotel, Nairobi.
Magavana Lee Kinyajui (Nakuru), Muthomi Njuki (Tharaka-Nithi) na seneta wa Kirinyaga Charles Kibiru pia walikuwepo katika mkutano huo.
Kenneth anatayarishwa kuwa mgombea mwenza au kwa nafasi ya ngazi ya juu serikalini katika muundo mpya wa utawala wa kisiasa utakaoundwa endapo mapendekezo ya BBI yatapitishwa.