Mbunge aandamana na wake zake 4 na watoto 27 Bungeni kuthibitisha uwezo wake

0Cqi0Z-1.jfif
0Cqi0Z-1.jfif
Mwanamume mmoja Mnigeria ambaye anawapenda wake zake wote bila kubagua amewaacha watu wengi wameduwaa baada ya video yake akiwatambulisha wapenzi wake bungeni kusambaa.

Alhassan Ado Doguwa anajivunia kuwa baba ya watoto 27 na ana wake wanne ambapo hujigamba nao kila mahali.

Katika video ya kusisimua iliyopakiwa na Gavana wa Nairobi, Mike Sonko,kiongozi huyo wa wengi katika Bunge la Kitaifa la Nigeria, anaonyeshwa akiwaomba wake zake wasimame.

Wanawake hao wanne ambao nyuso zao zilikuwa zimejaa tabasamu walisimama na kupunga mikono.

Kiongozi huyo alikuwa anajaribu kuwaonyesha wabunge wenzake kuwa ni mtu mwenye nguvu pande zote na wake zake wanne ni thibitisho kuwa ni mwanamume kamili.

Doguwa alikuwa amerejea tu bungeni baada ya kushinda uchaguzi mdogo na kutaka kurejea kwake kuwacha historia.

Kiongozi huyo ambaye ushindi wake wa awali ulikuwa umefutwa, aliwataka viongozi wenzake kutambua kwamba anazingirwa na nguvu za uongozi popote aendapo.

“Bwana Spika, ningependa kukujuza kwamba hii leo pamoja nami ni wake zangu wanne wapendwa, Halima waeza kusimama, Umma simama,” Ado alisema.

Alianza kujigamba kwamba barafu hao wa moyo wake wamemzalia watoto 27 warembo na tena wenye afya ambapo pia ni ishara ya mamlaka kulingana na Ado.

“Na sababu nyingine ni kukujuza kwamba wakati wananiita mtu mwenye nguvu, mimi sina mamlaka bungeni pekee lakini pia nina mamlaka nyumbani kwa sababu ninakabiliana na wake wanne," aliongezea Ado.