Klabu ya Talanta iliandikisha ushindi wa pili msimu huu baada ya kuifunga Ulinzi Stars 1-0 kwenye Uga wa Kenyatta, mjini Machakos.
Enock Machaka aliiweka Talanta kifua mbele kupitia bao alilopachika wavuni mnamo dakika ya 36.
Ulinzi, ambao walimletea mshambuliaji Enosh Ochieng katika dakika za mwisho, walikaribia kusawazisha wakati Brian Kafero alipiga mwamba wa goli zikiwa zimesalia dakika sita.
Kichapo hicho kilikuwa cha tatu kwa vijana wa Dunstan Nyaudo msimu huu.
"Nilikuwa nimeionya timu yangu kuhusu kucheza timu ambayo ilikuwa na hamu ya kupata pointi na ikaja kutuuma," Nyaudo alisema.
“Huyu itabidi nijilaumu kwa hilo. Tulizidiwa katika safu ya kiungo na hiyo ni juu yangu kwa kutopata mbinu sawa. Nia yangu sasa iko kwenye Mathare United ijayo."
Ushindi huo uliwapeleka Talanta kukwea hadi nafasi ya 13 wakiwa na alama tisa, huku Ulinzi wakisalia nafasi ya 12 kwa alama 10.