Manny Pacquiao astaafu kutoka ndondi

Muhtasari

•Pacquiao anatambulika kama bondia bora wa kulipwa duniani, akishinda mataji 12 katika mikanda minane tofauti na ni bondia wa pekee kushikilia ubingwa wa dunia kwa miongo minne

•Bondia huyo anayeshikilia mataji ya uzani tofauti ni seneta nchini humo na tayari ametangaza nia yake ya kuwania urais katika uchaguzi wa mwaka 2022.

Bondia wa Ufilipino Manny Pacquiao
Bondia wa Ufilipino Manny Pacquiao
Image: REUTERS/Erik De Castro/File Photo

Bondia wa Ufilipino Manny Pacquiao ametangaza kustaafu mchezo huo ili kuangazia kazi yake ya siasa.

Bondia huyo anayeshikilia mataji ya uzani tofauti ni seneta nchini humo na tayari ametangaza nia yake ya kuwania urais katika uchaguzi wa mwaka 2022.

Katika pigano lake la mwisho bondia huyu mwenye umri wa miaka 42-alishindwa na bondia wa Cuba Yordenis Ugas mjini Las Vegas mwezi uliopita.

"Nilisikia kengele ya mwisho tu. Mchezo ulikua umeisha," alisema Pacquiao.

Katika video iliyowekwa katika mitandao ya kijamii, Pacquiao alielezea kustaafu kwake kama "uamuzi mgumu" katika Maisha yake, akiongeza kuwa ndondi ilimpatia "nafasi ya kupigana na umaskini" na "ujasiri wa kubadilisha maisha zaidi".

Pia aliwashukuru mashabiki wake, marafiki na wale wote waliomuunga mkono katika mchezo huo,hususan Mkufunzi wake wa muda mrefu Freddie Roach, ambaye alimtaja kama "familia yangu, kaka na rafiki".

"Sitasahau kile nilichofanya na kufanikisha maishani mwangu," alisema.

Pacquiao anatambulika kama bondia bora wa kulipwa duniani, akishinda mataji 12 katika mikanda minane tofauti na ni bondia wa pekee kushikilia ubingwa wa dunia kwa miongo minne.