MECHI ZA KIRAFIKI

K'Ogalo kupasha misuli dhidi ya Talanta na Posta

McKinstry alisema ameridhishwa na kasi ya wachezaji kuzoea falsafa yake ya ukocha.

Muhtasari

•Mabingwa hao wa zamani wa Kenya wana mechi mbili za kirafiki wikendi hii.

•Watatunishiana misuli na Talanta Jumamosi kabla ya kukabiliana na Posta Rangers Jumapili.

Kocha mkuu wa Gor Mahia Jonathan McKinstry
Kocha mkuu wa Gor Mahia Jonathan McKinstry
Image: GOR MAHIA

Kocha mkuu wa Gor Mahia, Jonathan McKinstry, anaamini mechi mbili za kirafiki walizopanga wikendi hii zitasaidia wachezaji wake kuimarisha umahiri wao.

McKinstry alisema ameridhishwa na kasi ya wachezaji kuzoea falsafa yake ya ukocha.

"Maandalizi ya msimu mpya yanaendelea na viwango vya siha vinaboreka kila siku. Wachezaji wanaendelea kuzoea mawazo mapya ya kimbinu," McKinstry alisema.

Mabingwa hao wa zamani wa Kenya wana mechi mbili za kirafiki wikendi hii. Watatunishiana misuli na Talanta Jumamosi kabla ya kukabiliana na Posta Rangers Jumapili.

"Hii itahakikisha wachezaji wetu wote wanapata dakika 70-90 za muda wa kucheza ambao utawaruhusu kuendelea kujenga utimamu wao na pia kuonyesha jinsi wanavyoweza kutumia mafunzo waliyojifunza kwenye mazoezi," McKinstry alisema.

Mabingwa hao mara 19 wa Ligi Kuu ya Kenya watakuwa wakisaka kutwaa tena taji hilo ambalo limewakwepa kwa misimu miwili sasa.

Majitu hao wa jadi wametawala vichwa vya habari kwa sababu zisizo sahihi siku chache zilizopita baada ya mwenyekiti wao Ambrose Rachier kukiri kuwa mwanachama wa kikundi tatanishi cha Freemason.

Katibu mkuu wa klabu Sam Ocholla, hata hivyo, alijitokeza kwa haraka kuitenga klabu hiyo na Freemason, akisisitiza kwamba uamuzi wa Rachier kujiunga na shirika hilo ulikuwa wa kibinafsi.