Chumba cha kulala alichotumia Messi Qatar kugeuzwa makavazi kumuenzi nyota huyo

Chuo cha Qatar kilitangaza kuwa vitu alivyokuwa akivitumia Messi vitabaki kama kumbukumbu katika chumba hicho.

Muhtasari

• Mali za Messi zitakuwa urithi kwa wanafunzi na vizazi vijavyo na shahidi wa mafanikio makubwa aliyoyapata Messi wakati wa Kombe la Dunia - Chuo hicho kilisema.

Chuo cha Qatar kufanya makavazi chumba cha Messi
Chuo cha Qatar kufanya makavazi chumba cha Messi
Image: Facebook

Chuo kimoja nchini Qatar kimetangaza kuwa kina mipango ya kugeuza chumba ambacho staa wa Argentina Lionel Messi alikuwa akitumia kama malazi yake wakati wa mashindano ya kombe la dunia kuwa sehemu ya makumbusho yaani makavazi.

Kupitia taarifa ambazo zimechapishwa na majarida ya kimataifa, chumba hicho katika chuo kimoja ambacho timu ya taifa ya Argentina ilikuwa inalala kilikuwa kinatumiwa na Messi pamoja na rafiki wake wa muda mrefu Sergio Aguero.

Jarida la Goal.com lilinukuu halimashauri ya habari nchini Qatar kuwa chumba hicho sasa hakitatumiwa na mtu yeyote bali kitageuzwa kuwa makavazi madogo kama njia moja ya kumuenzi Messi.

Vitu vyote ambavyo nyota huyo wa PSG alikuwa anavitumia katika chumba hicho vitabaki chumbani humo kama maonyesho ya kifahari.

"Chumba cha mchezaji wa timu ya taifa ya Argentina Lionel Messi hakitabadilika na kitabaki kwa wageni pekee na si kwa wakazi. Mali za Messi zitakuwa urithi kwa wanafunzi na vizazi vijavyo na shahidi wa mafanikio makubwa aliyoyapata Messi wakati wa Kombe la Dunia. ," alisema Hitmi al Hitmi, mkurugenzi wa mawasiliano na uhusiano wa umma katika Chuo Kikuu cha Qatar, GOAL.com ilinukuu gazeti la Qatar Al Sharq.

Argentina ilishinda Kombe lao la tatu la Dunia na la kwanza kwa Messi katika maisha yake ya soka baada ya ushindi mnono dhidi ya Ufaransa katika mchezo wa michuano ya 2022. Meneja wa klabu yake, Christophe Galtier, alikiri furaha ya kufikia hatua hiyo muhimu, lakini pia alitangaza kwamba mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 35 hatacheza PSG hadi katikati ya Januari.

Messi alipokea mpira wa dhahabu katika fainali ya Kombe la Dunia 2022 kwa kuwa mchezaji bora wa mashindano hayo. Alifunga mabao saba nyuma ya jumla ya mabao nane ya Kylian Mbappe. Mchezaji huyo wa Ufaransa alitunukiwa kiatu cha dhahabu kwa kuwa mfungaji bora wa michuano hiyo.

Wiki jana taarifa kutoka Argentina pia zilidai kuwa taifa hilo linatathmini hatua ya kuweka picha ya Mchezaji huyo kwenye noti za nchi hiyo kama njia moja ya kumuenzi kwa umahiri wake katika malimwengu ya soka.