Nahodha wa Ufaransa, Hugo Lloris astaafu soka ya kimataifa

Aliiongoza Ufaransa mara 121, ambayo ni rekodi ya taifa hilo.

Muhtasari

•Lloris alibainisha kuwa wakati mwafaka wa kuchukua hatua hiyo kubwa umewadia  baada ya kutoa kila kitu kwa timu ya taifa ya soka.

•Lloris anajiondoa katika kikosi cha Ufaransa baada ya kuwakilisha taifa hilo lake katika mechi 145. 

Nahodha wa Ufaransa Hugo Lloris
Image: HISANI

Nahodha wa timu ya taifa ya soka ya Ufaransa, Hugo Lloris ametangaza kustaafu kucheza soka la kimataifa, wiki chache tu baada ya nchi hiyo ya Ulaya kukosa Kombe la Dunia 2022 katika hatua ya fainali.

Mlinda lango huyo wa Tottenham Hotspurs mwenye umri wa miaka 36 wakati akizungumza kwenye mahojiano na L'Equipe alibainisha kuwa wakati mwafaka wa kuchukua hatua hiyo kubwa umewadia  baada ya kutoa kila kitu kwa timu ya taifa ya soka.

"Baada ya miaka kumi na nne ya kutetea shati hili, nadhani nimefikia mwisho. Niliamua kuacha kazi yangu ya kimataifa, kwa hisia ya kuwa nimetoa kila kitu," Lloris alisema katika mahojiano hayo ya siku ya Jumatatu

"Nadhani ni muhimu kutangaza hili sasa, miezi miwili na nusu kabla ya kuanza kwa kufuzu kwa Euro." alisema.

Lloris anajiondoa katika kikosi cha Ufaransa baada ya kuwakilisha taifa hilo lake katika mechi 145. Aliiongoza Ufaransa mara 121, ambayo ni rekodi ya taifa hilo.

Lloris alicheza mechi yake ya kwanza ya kimataifa akiwa na umri wa miaka 21 katika mchuano wa kirafiki dhidi ya Uruguay mnamo mwezi Novemba 2008. Mechi yake ya mwisho kucheza ilikuwa fainali ya Kombe la Dunia 2022 ambapo Ufaransa ilipoteza kwa Argentina kwa mikwanju ya penalti.

"Kuwa kipa wa Ufaransa kwa misimu 14 na nusu ni jambo kubwa, lakini pia inachosha kiakili na natumai kujiweka huru kwa muda kutaniruhusu kuendelea kucheza kwa kiwango cha juu kwa miaka michache zaidi," alisema.