Chelsea yatangaza uteuzi wa Lampard kama meneja wa muda

Wamiliki klabu walimkaribisha Lampard kwa furaha na kueleza imani yao kwake.

Muhtasari

•"Chelsea imetangaza kuwa Frank Lampard ameteuliwa kuwa Meneja Msimamizi hadi mwisho wa msimu," taarifa hiyo ilisema.

•Lampard anarejea Stamford Bridge zaidi ya miaka miwili baada ya kutimuliwa kutoka katika Klabu hiyo ya London.

Image: HISANI

Klabu ya Chelsea imethibitisha kurejea tena kwa meneja Frank Lampard.

Katika taarifa ya Alhamisi alasiri, klabu hiyo ilitangaza kuwa Lampard atahudumu kama kocha msimami hadi mwisho wa msimu wa 2022/23.

"Chelsea imetangaza kuwa Frank Lampard ameteuliwa kuwa Meneja Msimamizi hadi mwisho wa msimu," taarifa hiyo ilisema.

Wamiliki wenza Todd Boehly na Behdad Eghbali walimkaribisha nahodha huyo wa zamani wa klabu hiyo kwa furaha na kueleza imani yao kwake.

"Tunapoendelea na mchakato wetu kamili na wa kutafuta kocha mkuu wa kudumu, tunataka kuipa klabu na mashabiki wetu mpango ulio wazi na thabiti kwa muda uliosalia wa msimu. Tunataka kujipa kila nafasi ya kufaulu na Frank ana sifa zote tunazohitaji ili kutufikisha kwenye mstari wa kumalizia," Boehly alisema.

Mmarekani huyo aliweka wazi kwamba watamuunga mkono Lampard kwa yoyote atakayo ili kuhakikisha amesaidia klabu kung'aa tena.

Lampard anarejea Stamford Bridge zaidi ya miaka miwili baada ya kutimuliwa kutoka katika Klabu hiyo ya London.

Chelsea iliafikia kumkabidhi mchezaji huyo wake wa zamani kazi hiyo baada ya kumpiga kalamu Graham Potter siku chache zilizopita.

The Blues walimtimua kocha mkuu Graham Potter siku ya Jumapili, takriban miezi saba tu baada ya kujiunga nao. Hii ni kufuatia msururu wa matokeo hafifu ambayo klabu hiyo imekuwa ikiandikisha katika wiki za hivi majuzi.

Katika taarifa yao, Chelsea walitangaza kwamba mkufunzi huyo mwenye umri wa miaka 47 alikubali kuondoka katika klabu hiyo. 

"Graham amekubali kushirikiana na klabu kuwezesha mabadiliko mazuri," taarifa ya klabu hiyo ilisoma.