Afueni kwa Jadon Sancho huku Borussia Dortmund ikimuokoa, yamrejesha kutoka United

Mkataba uliokubaliwa na klabu hizo mbili una thamani ya pauni milioni 3.4.

Muhtasari

•Jadon Sancho amejiunga tena na Borrusia Dortmund ya Ujerumani baada ya kupoteza nafasi yake ya kucheza Manchester United.

•Sancho alitaka sana kuondoka United na hata ndiye aliyesukuma kabisa uhamisho huo wa kwenda kujiunga na Borussia Dortmund.

Jadon Sancho
Jadon Sancho
Image: X

MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Uingereza, Jadon Sancho amejiunga tena na Borrusia Dortmund ya Ujerumani baada ya kupoteza nafasi yake ya kucheza Manchester United.

Sancho ambaye alijiunga na Mashetani Wekundu mwezi Julai 2021 anatarajiwa kusafiri hadi Ujerumani wakati wowote kuanzia leo baada ya upande wa Ten Hag kufikia makubaliano ya mkopo na Borrusia Dortmund siku ya Jumatano alasiri. Mkataba huo hata hivyo haujumuishi chaguo la kununua.

Mkataba uliokubaliwa na klabu hizo mbili una thamani ya pauni milioni 3.4 na klabu ya Borrusia inatarajiwa kugharamia sehemu ya mshahara wa mshambuliaji huyo.

Haya yanajiri miezi kadhaa baada ya winga huyo mwenye umri wa miaka 24 kutofautiana na kocha wa Manchester United, Erik Ten Hag, na kupelekea kutengwa kutoka kwenye kikosi hicho.

Inaripotiwa kuwa mchezaji huyo wa kimataifa wa Uingereza alitaka sana kuondoka United na hata inasemekana ndiye aliyesukuma kabisa uhamisho huo wa kwenda kujiunga na Borussia Dortmund.