Mwanamme aliyeachwa na jeneza la mkewe Meru kuishtaki serikali

Masaibu aliyopitia  Charles Mwenda ni kama ya mtu kuitazama filamu ya kuogofya kwani wakati serikali ilipokosa utu na kutekeleza vikali sheria ya kuwazuia watu wengi kusafiri kutoka baadhi ya sehemu za nchi ili kuzuia usambaaji wa virusi vya corona aliachwa pekee yake akinyeshewa na jeneza la mkewe  baada ya polisi kuzuia msafara wao na kuwarejesha  walikotoka waombolezaji waliokuwa wameandamana naye.

Mwenda sasa anataka kufidiwa na serikali  baada ya unyama huo ambapo alilazimika kusalia nje ya kituo cha polisi huku yeye pamoja na mwili wa mkewe katika jeneza wakinyeshewa  na mvua.

Amewasilisha kesi katika mahakama kuu ya Meru  akidai haki zake za kimsingi zilikiukwa  kwa ajili ya yote aliyopotia nje ya kituo cha polisi cha Kianjai

Anaitaka mahakama kuamuru kwamba   polisi walimfanyia ukatili licha ya yeye kutii kanuni za kukabiliana na COVID 19 ambazo serikali ilikuwa imetangaza.

Ameeleza jinsi yeye pamoja na waombolezaji wengine 31  walivyopewa idhini ya kusafiri kutoka Malindi hadi Meru  kwa mazishi ya mke wake  Faith Mwende aliyefariki  Mei tarehe 24 mwaka huu  lakini walipofika katika soko la  Keeria  walisimamishwa na polisi  na waombolezaji hao 31 wakiwemo watoto wake wawili kuagizwa kurejea Malindi.

Kikosi cha polisi waliojihami kisha kilimuagiza  Mwenda kuabiri gari la polisi pamoja na jeneza na mkewe na  kumpeleka katika kituo cha polisi cha Kianjai. Amesimulia jinsi wakati wa usiku alivyowarai polisi kumsaidia kuusafirisha mwili wa mke wake hadi kijijini mwao ,umbali wa kilomita tano lakini walikataa.