OFF THE HOOK: Mahakama ya Voi yafutilia mbali kesi ya Sonko Kumshambulia Kamanda wa polisi

Mahakama ya Voi imefutilia mbali mashtaka dhidi ya  gavana wa Nairobi Mike Sonko aliyefikishwa kortini kwa  kumshambulia kamanda wa polisi wa Pwani Yakubu Rashidi.

Katika uamuzi wake hakimu mkuu mkaazi  Fredrick Nyakundi alisema mlalamishi hataki tena kuendelea na kesi hiyo na hivyo Sonko hangejibu mashtaka hayo. Mkurugenzi wa mashtaka ya umma alikuwa amewasilisha ombi la kuitaka  mahakama kutupilia mbali kesi hiyo baada ya Yakubu kuamua kuachana nayo .

Stakabadhi ya mashtaka ilisema  Sonko alimshambulia afisa mmoja mkuu wa polisi mwendo saa sita unusu  wakati polisi huyo alipokuwa akitekeleza kazi yake  kinyume na  ibara ya 103 ya sheria ya huduma kwa polisi ya mwaka wa 2011 . Sonko alishtumiwa kwa kumpiga teke  kamanda wa polisi wa eneo la pwani Rashid  Yakubu katika uwanja mdogo wa ndege wa Ikanga .

Mashahidi wanne  akiwemo Yakubu na maafisa wa polisi James Mwanzia, Michael Muriithi,  Fred Sabai, Stephen Mtawa na Ibrahim Ahmed   walikuwa wameorodheshwa kutoa ushahidi dhidi ya Sonko.

Kisa hicho kilitokea Disemba tarehe sita  wakati gavana huyo alipokuwa akikamatwa katika kizuizi kimoja cha barabarani ili kujibu mashtaka ya ufisadi katika kaunti ya Nairobi. Sonko anakabiliwa na jumla ya mashtaka 19 ya ufisadi, utumiaji mbaya wa maalaka ya afisi yake na malipo yasio halali ya shilingi milioni 357.