Kwa Shelly Wacu kutoka Nakuru, ndoa yake ya miaka saba bila mtoto ilimfanya kuwa tayari kufanya jambo lolote ili afanikiwe kumzalia mumewe mtoto lakini baadaye matokeo yake yamekuwa majuto. Baada ya kujaribu njia zote za matibabu na hata miti shamba, shelly hakuweza kupata mtoto na haikuwa rahisi kwake kukubali kwamba yeye ni tasa . Watu wengi sana wakiwemo jamaa na rafiki zake walimtembeza Shelly kwa watu mbalimbali. Sio waganga, sio waomabaji na watalaam aina nyingi ili kumsaidia shelly apate mtoto lakini bila mafanikio. Kiasi cha pesa ambacho pia yeye na mumewe walitumia ili kuweza kupata mtoto kilikuwa cha juu sana na hatimaye mume wake alisalimu amri na kukubali kwamba hangewahi kupata mtoto, lakini kwa Shelly , vita vyake vya kuzaa havikuishia hapo .
Aliendelea kutafuta msaada kwa kila aliyemwambia kwamba kuna mtu anayeweza kumsaidia apate mtoto na ikawa rahisi sana kumshawishi kufanya chochote .Hapo ndipo ngoma ilipoanza wakati mhuburi mmoja wa kanisa jipya mjini Nakuru alipokuja na kupata sifa za kuweza kusuluhisha mambo mengi ikiwemo mtu kukosa mtoto .Wafuasi wake mjini Nakuru walimuita kuwa nabii na wanawake kwa wanaume waliokuwa na msururu wa matatizo mbalimbali walipiga foleni katika kanisa lake kupata msaada . Hapo ndipo Shelly alipoamua pia kucheza kamari ajaribu kupata usaidizi wa mhubiri huyo ili apate mtoto .
Alipokutana na mhubiri huyo, hakuna kilichomfanya ashuku kwamba alikuwa mlaghai na akamuombea na kumtaka awe na imani kwamba siku moja atapata mtoto . Kisha akampa ratiba ya kuja kwa maombi kila jumapili na hata siku ambazo watu hawakuwa kanisani ili aombewe . Kimoja baada ya kingine, siku moja mhubiri akamwambia kwamba lazima ashiriki naye mapenzi ndiposa ndoto yake ya kupata mtoto itimie . Washirika wengine wa kanisa hilo walijitokeza na kumuambia Shelly kwamba afanye kila anachoambiwa na nabii na angeweza kupata mtoto . Kuna waumini wa kanisa hilo waliojitokeza katika ushuhuda kanisani wakidai kwamba hakuwa na watoto lakini baada ya usaidizi wa nabii waliweza kufanikiwa kupata watoto .Hilo lilimpa sana matumaini Shelly kwamba siku moja angepata mtoto .
Baada ya kutafakari pendekezo hilo la mhuburi huyo kutaka kulala naye ili aweze kupata mtoto, Shelly alihofia kumwambia mume wake kuhusu hatua hiyo akiogopa kwamba angekataa. Kwa hivyo, alipiga moyo konde na kulala na mhubiri akiwa na matumaini kwamba atapata mtoto .Ole wake! Kilichofanyika baadaye sio tu cha kuhuzinisha bali ni jambo la kuvunja moyo kwani ufichuzi ulitolewa kwamba mhubiri huyo alikuwa keshafanya hivyo kwa wanawake kadhaa mbeleni na kwamba utabiri wake ni ulaghai ! Shelly alijua kweli amejiingiza katika shimo ambalo hangweza kujitoa . Muda sio mrefu uvumi ulianza kuzagaa jinsi ambavyo yeye na mhubiri huyo walilala pamoja na hata walikuwa wapenzi . Kabla hajajua cha kufanya mume wake alikuwa tayari keshaarifiwa kuhusu alichofanya na huo ndio uliokuwa mwisho wa ndoa yake . Mhubiri alianza kutafutwa na polisi kwa makosa mengi ya ulaghai baada ya watu kadhaa kujitokeza na lalama mbalimbali .Baadaye Shelly alilazimika kurejea kwao akiwa na mzigo wa aibu za kulala na mhubiri , fedheha ya kuachwa na mumewe na kuonekana kama mjinga aliyehadaiwa ili kulala na mhubiri feki .