Samaki mwenye hasira asaidia polisi kuwakamata wauza dawa za kulevya

sili
sili

Polisi nchini Australia wanaamini wamewakamata wanachama wa mtandao wa kimataifa wa wauza dawa za kulevya - kwa msaada wa mnyama mwenye hasira wa baharini aitwaye sili.

Maafisa wa polisi awali walidokezwa kuhusu uwepo wa watu kwenye moja ya visiwa vidogo baada ya boti ya washukiwa hao kuyia nanga magharibi mwa nchi hiyo.

Mtandao huo wa wafanyabiashara hiyo haramu unahusisha raia wa Australia, Marekani, Uingereza na Ufaransa.

Polisi pia wamefanikiwa kukamata dawa za kulevya zenye thamani ya dola 688,000.

Jumla ya watu watano wanashikiliwa na polisi na tayari wameshapandishwa kizimbani.

Kamishna wa polisi Chris Dawson ameviambia vyombo vya habari kuwa kukamatwa kwa washukiwa hao na dawa zao ni mafanikio makubwa.

"Tumeutikisa mtandao mkubwa na wa kimataifa wa biashara za dawa za kulevya hapa," amesema kamishana huyo na kuongeza kuwa wanaendelea kushirikiana na jumuiya ya kimatiafa katika kukusanya ushahidi wa kesi hiyo.

Watu wawili kati ya watano waliokamatwa walizuiliwa kukimbia kupitia njia ya bahari na mnyama huyo mkubwa mwenye hasira.

Washukiwa hao waliingia kwenye kisiwa kidogo kwa msaada wa boti ndogo na kuficha dawa hizo - ikiwemo kokeni chini ya majani ya mwani.

Baada ya kugundua kuwa uwepo wao kisiwani hapo umebainika, wakajaribu kukimbia kuelekea kwenye boti yao - ndipo walipokutana na "sili mkubwa mwenye hasira" aliyezuia njia yao.

"Walimwamsha, na akaruka kwa hasira na kuwatisha kwa kifua chake kikubwa," shuhuda mmoja ameiambia ABC radio.

"Jamaa hao kiuhalisia walikuwa na machagua mawili, kumvaa sili huyo hatari ama kukubali kushikwa, na wakafanya maamuzi ya kukubali kukamatwa."

-BBC