Antony Macharia alikanusha mashtaka hayo mbele ya hakimu mkuu Charles Mwaniki. Macharia anashtumiwa kwa kutekeleza kosa hilo Juni tarehe 9 mwendo wa saa nne usiku mtaani Lang’ata, Nairobi. Abiria huyo aliyedhulumiwa na Macharia ni mwanamke mwenye umri wa miaka 24 aliyetambulia na stakabadhi za mahakama kama MA.
Kulingana na ripoti ya polisi mteja huyo aliitisha huduma za teksi ya Uber akiwa katika barabara ya Crescent Road na ilipowasili aliketi katika kiti cha nyuma. Mwathiriwa alikuwa akiburudika na wenzake kabla ya kuitisha teksi hiyo na alipokuwa safarini kuelekea kwa mpenzi wake alihisi ni kana kwamba mtu alikuwa akimgusa. Muda mfupi baadaye alijihisi kuwa mnyonge. Alishangaa kujipata akiwa katika kiti kilicho kando ya dereva ambaye mikono yake ilikuwa ikimshika sehemu zake za siri.
Alishawishi dereva huyo kumpeleka katika nyumba ya mpenzi wake na walipofika alishuka na kupiga ukemi ili kupewa usaidizi. Mpenzi wake alitoka nje kutoka nyumba yake kwani tayari alikuwa amearifiwa na mwanamke huyo kupitia ujumbe wa sms.
Alipomueleza mpenzi wake kilichofanyika, alijaribu kutafuta maelezo kutoka kwa dereva huyo wa Uber aliyekana madai hayo na kupelekea ripoti kufikishwa kwa polisi. Mshukiwa aliachiliwa kwa dhamana ya shilingi laki tatu au bondi ya shilingi elfu 50 pesa taslimu. Kesi hiyo itaendelea Julai tarehe moja.