Mwanamume huyo aliyekuwa na ugonjwa wa kisukari pia alikuwa amelazwa katika kitengo cha wagonjwa mahututi (ICU) cha Hospitali ya Aga khan na alifariki alhamisi alasiri.
Taarifa kutoka kwa wizara ya Afya imesema alikuwa akiugua kisukari na aliwasili nchini tarehe 13 Machi kutoka Afrika Kusini kupitia Swaziland.
Wakati huo huo kenya imeripoti visa 3 zaidi vya ugonjwa huo nchini na kufikisha 31 watu walioambukizwa Corona hadi kufikia leo.
Wizara ya afya kupitia kwa afisa mkuu msimamizi Mercy Mwangangi ilithibitisha kuwa taifa la Kenya limesajili visa vitatu zaidi vya Coronavirus na kufanya idadi ya watu walioathirika na virusi hivyo kufikia watu 31.
Wizara hiyo pia ilisema watu 906 wanaosemekana kukaribiana na waathiriwa wa virusi hivyo wanasakwa na serikali huku 123 wakiwa wameruhusiwa kutoka hospitalini baada ya kufanyiwa vipimo.
Watu 18 nao wamelazwa katika hospitali ya Mbagathi wakisubiri kufanyiwa vipimo na madaktari.
Kaunti ambazo zimeripoti visa hivyo vya Corona kulingana na wizara hiyo ni; Nairobi, Kilifi, Kwale, Mombasa na Kajiado.
Watatu hao waliopatikana na virusi hivyo wote ni wakenya wawili kutoka kaunti ya Kilifi na mmoja kutoka kaunti ya Nairobi.
Watu zaidi ya 2000 waliofika nchini Jumatatu wameambiwa wajitenga ili kuzuiya kusambaa kwa virusi hivyo kwa watu wengine.
Mhariri: Davis Ojiambo