Ndoa yao ya miaka 7 sasa ilikuwa hatarini na juhudi zake za kutafuta msaada wa wazazi wa pande zote, viongozi wa kidini na hata rafiki wao wa karibu hazikuzaa matunda .
"Alianza ujeuri ambao sikujua ulitokea wapi, alipuuza kila nilichomuambia na sasa ikawa kila mtu anajifanyia mambo yake," alisema Geoff .
Wiki mbili zilizopita walikuwa wamelumbana kuhusu hatua ya Jebet kutaka kujilinganisha kimaisha na jirani zao. Mke wake hakuwa amefahamu kwamba maisha ya kila mtu ni tofauti kwa hivyo alikuwa akimpa presha mume wake kumfanyia vitu ambavyo majirani walikuwa wakiwafanyia wake zao.
"Kila alipojua mke wa jirani amenunuliwa nguo na mumewe, basi naye pia alitaka nimnunulie nguo, hakutaka kujua iwapo nilikuwa na pesa au la," alisema Geoff .
Malumbano yao kuhusu ushindani wa Jebet yalisababisha mgogoro katika ndoa yao na ikawa vigumu kwa Geoff kumridhisha kwa sababu alivyotaka vilikuwa vingi kwa wakati mmoja na hata vya gharama ya juu ambayo hangeweza kumudu. Matokeo yake –kununa kila wakati na wakajipata wanalala katika vyumba tofauti .
Hata hivyo , Geoff anakumbuka kwamba kuna kitu alichoshuhudia lakini hakukiwaza sana au kukichukuliwa kwa uzito wakati huo. Kakake mdogo James alikuwa akija nyumbani kwake kila mara kuwatembelea yeye na mkewe. Aligundua kwamba mke wake na ndugu yake walikuwa na urafiki mzuri kwa sababu licha ya matatizo katika ndoa yao, Jebet alikuwa akimkaribisha vizuri na kumfanyia maandalizi James wakati alipokuja kuwatembelea.
Katika fikra zake alijiambia ni mashehemji hao tu hapakuwa na la ziada – Kumbe ngoma ilikuwa ikichezwa! Usiku mmoja mke wake akilala , Geoff kwa sababu ya kuwa tu na shauku alitaka kujua Jebet amekuwa akizungumza na nani kila mara kupitia jumbe za sms na katika whatsapp. Alipoifungua simu ya mkewe alipatwa na mshutuko kugundua kwamba mke wake alikuwa ameihifadhi nambari ya kakake James kama ‘sweet love’.
Alishangaa mbona mkewe alikuwa akimuita ndugu yake jina hilo lililoashiria kuwepo uhusiano zaidi wa kindani. Alikumbuka jinsi wawili hao walivyokuwa wakiangaliana wakitabasamu tabasamu kila walipoonana. Hakujali kuhusu gumzo zao wakati huo lakini sasa taswira nzima ya kilichokuwa kikifanyika ilimjia .
Hamaki ilimsakama pale akijiuliza cha kufanya. Mkewe alikuwa amelala hajui kinachofanyika lakini Geoff alitamani kumuamsha wakati ule ili apate majibu ya maswali yake kutoka kwake. Akaamua kesho atafanya kikao na mkewe ajue ukweli lakini tayari alikuwa ameshathibitisha hofu yake kwamba kweli mkewe na kakake walikuwa wapenzi.
Geoff alipomkabili mkewe kumuuliza maswali, alipatwa na pigo kwa sababu mkewe hakukana bali alisema ni kweli yeye na James, kaka ya mumewe wamekuwa katika uhusiano wa kisiri kwa muda sasa. Mke wake aliendelea kumuambia kwamba James alikuwa akimjali sana kwa sababu alifanya kila juhudi za kumpa vitu alivyotaka.
Wakiendelea kujibizana, Jebet aliingia chumbani akachukua vitu vyake vyote na kuondoka. Alisema hatomrudia mumewe na kwamba wamepanga kuanza maisha upya na James.
Geoff alisononeka na kuhisi uchungu wa kusalitiwa na kakake pamoja na mke wake. Aliwaza kuhusu hatua atakayochukua lakini kama ilivyofanyika baadaye alisema uchungu wake kamwe hautamzuia pia kulipiza kisasi !
Alikumbuka kwamba Jebet alikuwa na dadake, aliyekuwa akimfuata na ambaye wakati mwingi alikuwa akija kuwatembelea. Alikata kauli ya kumtongoza ili awe katika uhusiano naye kama njia moja ya kumkwaza mke wake.
"Aliamua kutoroka na kaka yangu, mimi sasa nitamchukua dadake ili apate uchungu kama niliyopitia," alisema Geoff .
Visa hivyo havikuwafurisha jamaa zao na juhudi za kuwapatanisha hazikuwahi kufua dafu huku Jebet akiendelea kuishi na kaka ya mume wake naye Geofee akiishi na dada ya mke wake .