Uamuzi wa kusitisha shughuli za kaunti ulikuwa wa baraza la magavana si wa Oparanya, COG yasema

Baraza la magavana limefafanua kuhusu uamuzi wa kusitisha shughuli katika kaunti zote 47 kuanzia leo Alhamisi, Septemba 17.

Katika taarifa, baraza la magavana lilisema kwamba uamuzi huo haukufanywa na mwenyekiti wao Wycliffe Oparanya  kama ilivyo daiwa na maseneta.

“Kusitishwa kwa oparesheni si uamuzi wa mwenyekiti wa baraza…huu ni uamuzi uliyoafikiwa na baraza hilo Septemba 8, kutokana na kuchelewa kupitishwa kwa sheria ya mfumo wa ugavi wa mapato mwaka 2020," taarifa ya COG ilisema.

Taarifa hiyo inasema kwamba wafanyikazi wa kaunti wamekuwa wakitoa huduma kwa miezi mitatu bila mshahara kutokana na utata unaozingira mfumo wa ugavi wa mapato.

“Baadhi ya hawa wafanyikazi wamefukuzwa majumbani mwao kwa kutolipa kodi, hakuna pesa za kununua chakula na kulipia mahitaji mengine.”

Baraza hilo lilisema kwamba taasisi za afya katika kaunti hazina dawa, hakuna pesa za kununua vifaa vingine muhimu au hata pesa za kulipia gharama zingine.

“Serikali za kaunti zinadaiwa jumla ya zaidi ya shilingi bilioni mbili gharama za umeme kipindi cha matumizi ya pesa cha mwaka 2020/2021.”

Magavana pia wameshtumu maseneta kwa kushindwa kulinda maslahi ya serikali za kaunti.

“Inaonekana maseneta wameamka kutoka usingizi waliyokuwa wamelala kwa miaka mitatu iliyopita. Walijua kuhusu mfumo mpya wa ugavi wa mapato miaka mitatu iliyopita na ilhali wamekuwa wakichezea shere nchi wakati wakiahirisha vikao vya kujadili mfumo huo mara kumi”

Baraza hilo lilisema kwamba halitendelea kuomba lisikizwe ila tu kusitisha huduma za kaunti zote, likitarajia muafaka kupatikana ili kuzuia athari za kutokuwepo kwa huduma muhimu.

Maseneta siku ya Jumatano walishambulia sana baraza la magavana kutokana na hatua ya kutangaza kusitisha oparesheni zote za kaunti.

Maseneta walimtaja Oparanya kama msaliti, muongo na anayeongoza kikundi cha vijana 'club of boys' chenye lengo la kushambulia idara inayotetea ugatuzi.