Ruto atashinda,Raila hatakubali kushindwa katika uchaguzi wa Agosti-Shollei

Muhtasari
  • Kulingana na Shollei, Naibu Rais William Ruto atashinda uchaguzi wa urais naye Raila atawasilisha ombi kuupinga
GLADYS SHOLLEI
Image: GLADYS SHOLLEI/TWITTER

Mwakilishi wa wanawake wa Uasin Gishu Gladys Shollei amesema mgombeaji wa Azimio la Umoja Raila Odinga hatakubali kushindwa katika uchaguzi wa Agosti 9.

Kulingana na Shollei, Naibu Rais William Ruto atashinda uchaguzi wa urais naye Raila atawasilisha ombi kuupinga.

"Historia itajirudia na Raila amekuwa akiwasilisha ombi la kupinga uchaguzi mwingine wowote ambao ameshiriki na kushindwa,tunatumai atatimiza ahadi yake ya kukubali kushindwa katika uchaguzi ujao," aliambia Citizen TV Jumatano.

Shollei alisema kuwa Raila hajawahi kukubali matokeo yoyote ya uchaguzi na kwa hivyo, Kenya Kwanza iko tayari kushughulikia ombi lake kwa sababu wanaamini katika sheria.

Raila amepinga matokeo ya uchaguzi wa urais mara tatu katika 2007, 2013 na 2017 akidai aliwashinda washindani wake.

Akizungumza Jumanne, Raila katika mahojiano na vituo vya televisheni alisema kwamba atakubali kushindwa na kumpongeza mshindi.

"Kwa hakika, mimi ndiye mwanaspoti kati yangu na yeye (Ruto) na najua asiyekubali kushindwa sio mshindani," Raila alisema..