Serikali yatangaza Jumanne, Agosti 9 wiki ijayo siku kuu ya kitaifa

Wakenya siku ya Jumanne watakuwa wanatekeleza haki yao ya demokrasia kuwachagua viongozi wao.

Muhtasari

• Wakenya siku ya Jumanne watakuwa wanatekeleza haki yao ya demokrasia kuwachagua viongozi wao.

Waziri wa usalama Fred Matiang'i
Image: FRED MATIANG'I/TWITTER

Waziri wa usalama wa ndani Fred Matiang'i ametangaza kuwa Jumanne wiki ijayo itakuwa sikukuu ya kitaifa.

Katika notisi ya gazeti rasmi la serikali ya tarehe 29 Julai na ambayo ilitolewa siku ya Alhamisi, Matiang'i alisema Jumanne itakuwa likizo ili kuwaruhusu Wakenya kushiriki katika Uchaguzi Mkuu.

“Inaarifiwa kwa taarifa kwa umma kwamba Waziri wa Mambo ya Ndani, kwa mujibu wa na kutekeleza mamlaka aliyopewa na kifungu cha 2 (4) cha Sheria ya Sikukuu za Umma, ikisomwa pamoja na Ibara ya 101 ( 1), 177 (1) (a) na 180 (1) ya Katiba ya Kenya 2010, anatangaza Jumanne, Agosti 9, 2022 kuwa sikukuu ya umma..." ilisoma notisi ya gazeti la serikali la Julai 29, 2022.

Siku ya Jumanne wakenya wote watakuwa wanatekeleza haki yao kikatiba kuwachagua viongozi wao.

Wakenya watakuwa wakichagua rais, gavana, seneta, mwakilishi wa kike, mbunge na mwakilishi wa bunge la kaunti.