Wamatangi,Karungo Thangwa, Wamuratha watwaa ushindi Kiambu

Watatu hao walikabidhiwa vyeti vya ushindi usiku wa kuamkia Jumapili.

Muhtasari

•Kimani Wamatangi alitangazwa mshindi kama gavana mteule wa Kiambu baada ya kupata 348371 .

•Thangwa alitangazwa mshindi wa kiti cha useneta baada ya kuzoa kura 579411 dhidi ya mpinzani wake George Mara kura 112304.

baada ya kupokea vyeti vya ushindi mnamo Agosti 14, 2022.
Wamuratha, Afisa wa IEBC, Karungo Thang'wa na Kimani Wamatangi baada ya kupokea vyeti vya ushindi mnamo Agosti 14, 2022.
Image: AMOS NJAU

Gavana mteule wa Kiambu Kimani Wamatangi, seneta mteule Karungo Thangwa na mwakilisi wa wanawake mteule Ann Wamuratha wamekabidhiwa vyeti.

Zoezi hilo lilifanyika katika Kiambu institute of science and technology usiku wa kuamkia Jumapili.

Kimani Wamatangi alitangazwa mshindi kama gavana mteule wa Kiambu baada ya kupata 348371 huku Patrick Wainaina jungle akifuata kwa kura 273361, James Nyoro wa Jubilee 99562, Moses Kuria wa CCK 24512 huku William Kabogo wa Tujibebe Wakenya Party akifunga mkia kwa kura 106980.

Tayari Mbunge wa Gatundu Kusini Moses Kuria alikuwa amekubali kushindwa huku Wainaina jungle na James Nyoro wakiapa kuwasilisha ombi mahakamani kupinga ushindi wake (Wamatangi).

William Kabogo ambaye alikuwa akitafuta kurejea hajatoa tamko kuhusu mwelekeo ambao anaweza kuchukua.

Akihutubia wanahabari baada ya kutunukiwa cheti, Wamatangi aliwashukuru watu wote waliompigia kura.

Alisema atafanya kazi kubadilisha maisha ya watu wa Kiambu.

Alisema umoja wa chama cha UDA uliwafanya washinde kiti hicho kwa jinsi ulivyoratibiwa vyema.

"Ninaheshimu imani ambayo watu wa Kiambu wanayo kwangu na nitahakikisha kuwa nitaifanya kuwa bora," alisema.

Alisema kuwa ataanzisha miradi ya maendeleo ambayo itabadilisha maisha ya wakazi wa Kiambu.

"Ningependa kuwashukuru wanachama wa UDA na watu wote wa Kiambu kwa kunipa fursa ya kuwahudumia," alisema.

Aliwapongeza washindani wake na kuapa kufanya kazi pamoja nao na kuifanya Kiambu kuwa kuu.

"Ningependa kuwakaribisha washindani wangu wanaostahili kujiunga nami na kujenga Kiambu," alisema.

Alieleza imani kuwa mgombea wao wa urais William Ruto ataibuka mshindi na IEBC itamkabidhi cheti hicho.Kabla ya kuwania ugavana, Wamatangi amehudumu kama seneta wa Kiambu kwa mihula miwili mfululizo chini ya chama cha Jubilee.

Waliandamana na mbunge mteule wa Thika mjini Alice Ngang'a, Elijah Njoroge Alias Kururia (Gatundu Kaskazini)

Paul Karungo Thangwa alitangazwa mshindi wa kiti cha useneta baada ya kuzoa kura 579411 dhidi ya mpinzani wake George Mara kura 112304.

Akizungumza, Karungo Thangwa aliwashukuru wenyeji wa Kiambu kwa kumpa miadi ya kuwahudumia.

"Sitawaangusha watu wetu na ninaahidi kufanya kazi," alisema.

Ann Wamuratha alitangazwa wa kinyang’anyiro cha mwakilishi wa wanawake kwa kupata 405492.

Alisema atatumikia watu wa Kiambu kwa kumwamini kuwaongoza.