Ufichuzi:Jinsi Daktari alivyoiba moyo na figo za marehemu

Moses Njue
Moses Njue
 Daktari mmoja ameaiambia mahakama ya Meru jinsi mwanapatholojia wa zamani wa serikali Moses Njue alivyoiba moyo na figo za  mwanamme mmoja aliyeaga dunia bila ruhusa ya familia ya mwendazake  baada ya kumfanyia uchunguzi wa kufahamu kilichomwua .Dr Scholastica Kimani,  ambaye ni mwanapatholojia katika hospitali ya Meru level  V  amemwambia  hakimu mkuu mkaazi wa Meru  Evans Mbicha  kuhusu jinsi baada ya  kuufanyia upasuaji mwili wa mzee Benedict Karau, Dr Njue  alivifunga viungo vya marehemu ,moyo na figo  na kuondoka navyo .Dr Kimani  alikuwa akiiwakilisha serikali ilhali  Dr Njue alikuwa amepewa kazi na  Bi. Martha Gakuo  ambaye ni mjane wa tatu wa mzee Karau  aliyekuwa naye wakati alipoaga dunia Machi mwaka wa 2015 .

 Vipimo

Amesema Dr Njue, aliyekuwa ameandamana na wanafunzi kutoka chuo cha   Kings Medical College,  alinakili kwamba kifo cha Karau kilisababishwa na mshtuko wa moyo  kwa ajili ya uvimbe katika mshipa wa damu  ,lakini akasisitiza kwamba atauchukua moyo huo ili kuufanyia vipimo na kuthibitisha kikamilifu matokeo hayo .Dr Kimani  amesema mwanzoni alihofishwa  kwamba Dr Njue alikuwa akivibeba viungo hivyo kutoka kwa marehemu  bila ruhusa ya familia yake   lakini akajiambia labda Njue angewaeleza jamaa za marehemu baadaye . Ameiambia mahakama kwamba ingawaje mzee Karau alikuwa na majeraha yanayoonekana ,hayakuzingatiwa kama sababu ya kifo cha mzee huyo aliyekuwa na umri wa miaka 70.

Kabla ya kesi kuanza kusikizwa siku ya jumanne Bi.Martha Gokou  alitaka kesi hiyo kuahirishwa ili wakili wake afahamishwe kuhusu suala hilo  akisema kwamba alikuwa ametajwa pakubwa katika uchunguzi huo. Hata hivyo  upande wa mashtaka  ulifaulu  kukataa ombi  lake kwani mashahidi saba tayari walikuwa wamefika mbele ya  jopo la uchunguzi kutoa ushahidi wao na Bi Gokou hakuonyesha nia yoyote ya kutaka kumhusisha wakili wake . Wakili wa serikali Anthony Musyoka  pia amesema  kwamba mahakama haijatoa  uamuzi wa iwapo inafaa kumshtaki yeyote kuhusu kifo cha mzee  Karau .

Sumu

Dr Kimani  pia amesema walituma sampuli kwa mwanakemia wa serikali ili kufahamu iwapo mwendazake alipewa sumu . Ilikuwa ni baada ya familia kupitia wakili  Charles Mwongela,  kupata ruhusa ya kuufukua mwili wa marehemu  ili uchunguzi wa pili wa kubaini sababu ya  kifo  chake kufanywa ndipo walipomuuliza Dr.Njue kurejesha  moyo wa marehemu lakini  Njue akazidi kukwepa .Dr Njue tayari ameshtakiwa kwa  madai ya wizi wa  viungo hivyo  na uharibifu wa ushahidi .

Familia inadai kwamba kuondolewa kwa moyo na figo za marehemu ilikuwa njama ya kuficha ukweli kuhusu kilichosababisha kifo chake . Familia hiyo ilishauriwa na mtaalam kwamba majeraha ya kichwa yanaweza kusababisha kifo cha mtu wa umri wa juu na walitaka kuona endapo kulikuwa na majeraha  katika mwili wa marehemu kuonyesha iwapo alijaribu kujikinga alipokuwa akishambuliwa na mtu . Vikao hivyo vitaendelea Agosti Mosi .