Uganda yapanga kunyonga wapenzi wa jinsia moja

Waziri wa maadili nchini Uganda ametangaza mipango wa kuanzisha tena sheria inayopinga mahusiano ya jinsia moja, iliyofutwa na mahakama ya kikatiba mwaka 2014.

Waziri Simon Lokodo ameliambia shirika la habari la Reuters kuwa sheria hiyo mpya itamuadhibu hukumu ya kifo yeyote atakayeenda kinyume nayo.

''Sheria yetu ya sasa inatubana sana. Inasema kuwa kitendo hiki ni jambo la kuvunja sheria. Tunataka iwekwe wazi kuwa mtu yeyote anaepigia debe suala hili anaweza kushtakiwa. Wale wanaofanya vitendo vya kushangaza watahukumiwa kifo.''

Aliendelea kueleza kuwa, ''mahusiano ya aina hii sio kitu cha kawaida kwa watu wa Uganda na kumekuwa na waajiriwa wengi shuleni ambao ni wapenzi wa jinsia moja wanaowafundisha watu uongo kuwa mtu anazaliwa na hisia za mapenzi ya jinsia moja.''

Mwezi Februari mwaka 2014, Rais Yoweri Museveni alisaini muswada wa sheria wa kuwabana wapenzi wa jinsia moja lakini sheria hiyo ilifutwa na nahakama mwezi Agosti mwaka huo huo.

Mabadiliko hayo yalitokea baada ya kubainika kuwa wabunge walipitisha sheria hiyo bila kufuata utaratibu wa kisheria.

Bwana Lokodo amesema muswada mpya ambao utawasilishwa bungeni wiki zijazo unaungwa mkono na wabunge pamoja na Rais Museveni.

''Tumekuwa tukizungumza na wabunge na tumehamasisha idadi kubwa, wengi wao wanakikubaliana na jambo hili.''

Miaka mitano iliyopita nchi za Afrika Mashariki waliweka vikwazo na Marekani kwenye uombaji wa viza na wakasitisha utoaji msaada na mazoezi ya kijeshi.

Bwana Lokodo amesema kuwa nchi yake ipo tayari kwa mashambulio yoyote watakayoyapata juu ya kampeni hiyo.

''Hatupendi kutumiwa'' amesema waziri huyo.

''Tunajua kuwa kitendo hiki kitawachukiza watu wengi wanaotusaidia kwenye uongozi na masuala ya bajeti.

Hatuwezi kusikiliza watu ambao wanataka tukubali suala ambalo ni kinyume na maadili yetu.''

Kwa sheria za sasa hivi ambazo ni za kutoka enzi za utawala wa waingereza, mapenzi ya jinsia moja ni kosa ambalo watu wanaweza kupewa adhabu ya kifungo cha maisha na wanaharakati wanasema sheria hii mpya itaanzisha mashambulizi makali kwa watu wanaojihusisha na mapenzi ya jinsia moja.

Pepe Julian Onziema kutoka shirika la Sexual Minorities Uganda linalofanya kazi na mashirika mengi yanayounga mkono mapenzi ya jinsia moja, ameiambia Reuters kuwa wafanyakazi wake wamejawa na hofu.

''Sheria hii ilipotangazwa kwa mara ya kwanza, iliongeza chuki na ubaguzi,'' amesisitiza Bwana Onziema.

''Mamia ya watu ambao wanashiriki mapenzi ya jinsia moja wanalazimika kuhama nchi na kugeuka wakimbizi na wengi watafata endapo sheria hii itapitishwa. Itatufunga sisi kuonesha ushirikiano wetu hata kufanya kampeni za kuelimisha jamii.''

Bwana Onziema amesema wapenzi wa jinsia moja watatu na mmoja ambaye alibadilisha jinsia wameuawa ndani ya mwaka huu nchini Uganda, na wiki iliyopita mtu mmoja alipigwa hadi kufariki dunia kwa sababu ni mpenzi wa jinsia moja.

-BBC