Miili ya Mariam na mwanawe yapatikana ikiwa imekumbatiana

Miili ya Mariam Kigenda na mwanawe wa miaka minne Amanda ilipatikana ikiwa imekumbatiana katika kiti cha nyuma ndani mwa gari lao.

Siku ya Ijumaa wapelelezi walisema kuwa walikuwa na wakati mgumu kutenganisha miili hiyo.

Gari hilo lilikuwa katika hali ya kuegeshwa (parking mode)

Juhudi za kutafuta na kuokoa gari hilo ambalo lilianguka hadi mita 58 ndani ya bahari hindi ziliendelea kuanzia mnamo Septemba 29.

Ilikuwa tu siku ya kawaida ya Jumapili katika kituo cha ferry wakati gari la Kigenda liliteleza kutoka ferry aina ya MV Harambee na kutumbukia ndani mwa bahari.

Kilio cha kuomba msaada hakikufua dafu huku abiria wakitizama wasijue cha kufanya huku gari lao likitumbukia.

Kwa siku 13 misheni hiyo ilikuwa na kazi nyingi na ambayo ilihitaji utaratibu wa hali ya juu huku wapiga mbizi 80 wakishirikishwa kwenye shughuli hiyo.