VIDEO: Caster Semenya ajiunga na timu ya soka

semenya
semenya

Bingwa mara mbili wa Olimpiki katika mbio za mia 800 Caster Semenya amejiunga na timu ya soka ya wanawake nchini Afrika Kusini.

Mwanariadha huyo mwenye umri wa miaka 28 hawezi kushiriki katika mbio za mita 800 bila kutumia dawa za kupunguza homoni za kiume mwilini mwake sheria mpya ilioidhinishwa na shirika la riadha duniani IAAF.

Hatua hiyo inamaanisha kwamba hawezi kutetea ubingwa wake wa mita 800 mjini Doha mwezi ujao - ijapokuwa bado anapigania kubadilishwa kwa sheria hiyo kupitia mahakama.

Kwa sasa amejiunga na klabu ya soka ya wanawake iliopo Gauteng kwa jina JVW.

Bingwa huyo mara tatu ambaye alitangaza mwezi Julai kwamba hatotetea ubingwa wake katika mbio za mita 800 kwa kuwa hawezi kuanza kuichezea JVW hadi msimu wa 2020, baada ya kujiunga na timu hiyo nje dirisha la uhamisho.

''Ninatazama kuanza safari mpya , nashukuru mapenzi na uungwaji mkono niliopata kutoka kwa timu hii'', Semeya aliambia mtandao wa klabu hiyo.

JVW FC, ilibuniwa 2013 na nahodha wa timu ya taifa ya wanawake nchini Afrika Kusini Janine van Wyk, akitaka kuwatambua, kuwaimarisha na kuwafichua wachezaji wa kike.

Klabu hiyo ni miongoni mwa klabu kubwa katika ligi katika mkoa wa Gauteng - ligi kuu ya wanawake nchini Afrika Kusini imegawanyika katika makundi manane ya kimkoa.

Mmiliki wa klabu hiyo van Wyk aliambia BBC kwamba Semenya hajawacha kukimbia.

Alisema: Yuko katika mapumziko kwa wakati huu ndio maana ana muda wa kufanya kitu tofauti.

Ameshiriki mazoezi mara mbili na timu hii na unaweza kuona kwamba anajua kucheza soka lakini bado ni sharti kumsaidia kidogo kwa kuwa uchezaji ni tofauti na riadha.

Kumuona katika ligi hii ni jambo jema na nadhani wasichana wadogo watapata msukumo mkubwa kutoka kwa Caster.

Semenya sio mwanariadha wa kwanza kujiunga na kandanda - baada ya kustaafu 2017 , Usain Bolt alifanya mazoezi na klabu moja ya Norway Stromsgodset na nyengine ya Australia Central Coast Mariners, lakini hakupata kandarasi.

Semenya pia anafuata nyayo za Maria Mutola wa Zambia ambaye alijiunga na kandanda baada ya riadha.

IAAF iliamua kuweka sheria hiyo kwa madai kwamba wanariadha wanawake walio na homoni nyingi za kiume wana uwezo zaidi ya wenzao wa kike.

Wanariadha hao wametakiwa kutumia dawa ili kupunguza viwango vya homoni hizo ili kuweza kushiriki katika mita 400 hadi 1500 la sivyo waingie katika mbio nyengine ndefu.

https://twitter.com/i/status/1169314359996223491

-BBC