Patanisho: Mwanadada mwenye ujauzito wa miezi 3 amtema mumewe na kuolewa na mwingine

Mike alifichua kwamba ndoa yao imedumu kwa chini ya mwaka mmoja.

Muhtasari

•Mike alisema mke wake alienda nyumbani kwao takriban miezi miwili iliyopita na kufikia sasa amedinda kurudi nyumbani bila kutoa sababu yoyote.

•Mike alisema hadhani kuwa mke wake mjamzito alikuwa serious aliposema kwamba ameolewa na hivyo akaomba kusaidiwa kujua ukweli.

Ghost Mulee studioni
Ghost Mulee studioni
Image: RADIO JAMBO

Kwenye kipindi cha Gidi na Ghost Asubuhi, kitengo cha Patanisho, Bw Mike ,25, alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mke wake Hellen Nakisia, 22.

Mike alisema mke wake alienda nyumbani kwao takriban miezi miwili iliyopita na kufikia sasa amedinda kurudi nyumbani bila kutoa sababu yoyote.

"Mwaka jana Desemba niLImtumia pesa akuje kwenye niko. Baada ya kutuma alisema atakuja lakini hakuja. Siku iliyofuata nilimpigia simu nikamuuliza kwa nini hakuja. Aliniambia nishughulike na maisha yangu," Mike alisimulia.

Alifichua kwamba ndoa yao imedumu kwa chini ya mwaka mmoja na Hellen kwa sasa ana ujauzito wake wa miezi mitatu.

"Nimemtumia nauli mara mbili akuje lakini hajakuja. Sijawahi kujitambulisha kwao lakini kwetu anajulikana, hata amewahi kaa nyumbani," alisema.

Mike alifichua kuwa licha ya wao kutokuwa pamoja huwa wanazungumza mara kwa mara lakini mazungumzo yao hayakuwa mazuri hivi majuzi.

Alidai kwamba katika mazungumzo yao ya mwisho, Hellen alimfichulia kwamba tayari amejitosa kwenye ndoa nyingine.

"Tuliongea jana nikamuuliza ameamua aje.  Aliniambia kwamba amepata bwana. Aliniambia amekaa kwa hiyo ndoa siku tatu," alisema.

Mike alisema hadhani kuwa mke wake mjamzito alikuwa serious aliposema kwamba ameolewa na hivyo akaomba kusaidiwa kujua ukweli.

Hellen hata hivyo hakushika simu wakati alipopigiwa na Ghost na hivyo Patanisho haikuweza kuendelea.

Je, ushauri wako kwa Mike ni upi?