Patanisho: Mwanadada alia kutengwa na mamake "Anaambia watu hakutarajia kunizaa, anasema kwetu hawanitaki"

"Huwa simpigii mama simu, na yeye huwa hanipigii. Nilimpigia mara ya mwisho Disemba mwaka jana," Melvin alisema.

Muhtasari

•Melvin alisema uhusiano wake na mamake uliharibika mwezi Disemba mwaka jana baada ya yeye kuzozana na dadake mdogo. 

•Alimalizia kwa kumhakikishia mamake kuhusu upendo wake mkubwa kwake na kumuomba azungumza na dada zake.

Image: RADIO JAMBO

Melvin Makungo ,23,  kutoka Kakamega alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mama yake Jackline Isombi ambaye alikosana naye mwaka jana.

Melvin alisema uhusiano wake na mamake uliharibika mwezi Disemba mwaka jana baada ya yeye kuzozana na dadake mdogo. 

"Mimi ni mzaliwa wa kwanza.Dada zangu walizaliwa na baba mwingine. Mwaka jana, Disemba nilitoka Mombasa nikaja Nairobi. Mama ndiye alitaka nikuje. Dadangu mmoja akawa ananiibia nguo zangu nanyamaza, nikanunua simu akaniibia. Nikiambia mamangu ananiambia kwamba ata yeye alilelewa hivyo.

Mamangu akawa anaambia watu ata hakutarajia kunizaa, anaambia watu kwetu hawanitaki. Kwetu kuna wasichana watatu, na wavulana wawili nyuma yangu. Dadangu mmoja ndo alikuwa ananiibia. Mamangu anasema ni vile siwapendi, juu sijalelewa na wao ndo maana nalalamika," Melvin alisimulia.

Jaribio la kumpatanisha Melvin na mzazi huyo wake hata hivyo halikufua dafu kwani Bi Jackline hakupatikana kwa simu.

Melvin alisema, "Huwa simpigii mama simu, na yeye huwa hanipigii. Nilimpigia mara ya mwisho Disemba mwaka jana."

Aliendelea kulalamika, "Nilijaribu kuenda nyumbani nilichukua dadake mdogo. Dada yangu aliniibia simu, akauzia dada ya mamangu. Nilienda huko nikaiona, akasema dadangu ndiye aliwaletea. Nikamwambia simu ni yangu anirudishie. Vile walinirudishia nilichukua dada huyo wa mamangu tukaenda naye nikamueleza mamangu vile dadangu aliniibia simu, mamangu ata hakutaka kunisikia. Babangu namjua vizuri sana. Waliachana."

Alimalizia kwa kumhakikishia mamake kuhusu upendo wake mkubwa kwake na kumuomba azungumza na dada zake.

"Mama mimi bado nakupenda kama mamangu. Jaribu kuongelesha dada zangu. Ata kama wanaona mimi nilizaliwa nje ya ndoa, waniheshimu tu tuweze kuishi kama ndugu," Melvin alisema.