Patanisho: Jamaa apata mkewe ameandika namba za wanaume 10, ampigia mmoja na kutusiwa vibaya

"Nilikuwa nimeenda kazini. Kurudi kazini nilipata ameandika namba nyingi nikaweka. Zilikuwa number za wanaume," Joseph alisimulia.

Muhtasari

•Joseph alisema ndoa yake ya miaka mitano ilivunjika mwezi Aprili wakati mkewe alitoroka na kuwachukua watoto wao wawili.

•Joseph pia aliibua madai ya mkewe kutokuwa mwaminifu kwa ndoa.

Ghost na Gidi studioni
Image: RADIO JAMBO

Joseph Odanga ,24, kutoka Siaya alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mke wake Sylvia Odanga ,22, ambaye alikosana naye takriban miezi miwili iliyopita.

Joseph alisema ndoa yake ya miaka mitano ilivunjika mwezi Aprili wakati mkewe alitoroka na kuwachukua watoto wao wawili.

"Tumeishi naye miaka tano. Tulikosana tu mambo ya nyumbani. Nikimwambia afanye kitu kwa nyumba hataki. Nikienda kazi analeta wanaume kwa nyumba," Joseph alisimulia.

Aliendelea, "Ilianza 2021. Ukimuongelesha anakuwa mkali, anataka kukuchapa. Nilitaka kama mimi ndiye mwenye makosa anisamehe na arudi. Nilienda kwao mwezi wa sita tukaongea na wazazi wakaniambia nirudi tarehe kumi. Nilipoenda walisema nimchukue turudi na yeye. Yeye alitoka akaenda Nairobi.Huwa tunaongea lakini tukiongea anakuwa mkali."

Joseph pia aliibua madai ya mkewe kutokuwa mwaminifu kwa ndoa.

"Nilikuwa nimeenda kazini. Kurudi kazini nilipata ameandika namba nyingi nikaweka. Zilikuwa number za wanaume. Zilikuwa namba kumi. Alikuwa ameandika kwa karatasi. Niliwapigia simu. Kuna mmoja alishika akanitusi, nikaachana nao. Nikimuacha nyumbani naye anafanya mambo yake," alisema.

Juhudi za kumpatanisha Joseph na mkewe hata hivyo hazikufua dafu kwani Sylvia alikata simu yake wakati alipopigiwa.

Joseph alimwambia, "Bado nakupenda Sylvia. Urudi kama awali, tuishi pamoja na wewe."

Je, ushauri ama maoni yako ni yepi kuhusu Patanisho ya leo?