Jamaa akataa kumnunulia mkewe chochote, hata slippers licha ya kupata pesa nyingi

Cynthia alifichua kuwa mumewe alikuwa amemtelekeza na hakuwa akiwajibikia majukumu yake.

Muhtasari

•Kelvin alisema mkewe alitoroka na kuenda na watoto wap wawili bila hata kumweleza sababu yake kuchukua hatua hiyo.

•Cynthia alifichua kwamba Kelvin angepata pesa nzuri na hangemnunulia hata zawadi ndogo.

Gidi na Ghost
Gidi na Ghost
Image: RADIO JAMBO

Kelvin Wanjala alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mke wake Cynthia ambaye aligura ndoa yao ya miaka mitatu mwaka jana.

Kelvin alisema mkewe alitoroka na kuenda na watoto wap wawili bila hata kumweleza sababu yake kuchukua hatua hiyo.

"Ilikuwa mwaka jana, kurudi nyumbani nilipata bibi ameenda. Nilipiga simu kwao akaniambia nijipange nitafute bibi mwingine. Bado nasubiri aniambie msimamo wake. Mimi sikumbuki nikimkosea. Sijawahi kukosana na yeye," Alisema.

Cynthia alipopigiwa simu alifichua kwamba mumewe alikuwa amemtelekeza na hakuwa akiwajibikia majukumu yake.

"Hashughulikii majukumu ya nyumba. Hana haja ya mwanamke. Anataka tu wa nje. Watoto anashughulikia lakini mwanamke aliye naye kwa nyumba hawezi," alisema.

Aliongeza, "Nilikuwa naye miaka na hata hakuwa akiniruhusu kuenda kwetu. Sikuwa na simu, akipigiwa simu ya kwetu anakosa kuchukua."

Mama huyo wa watoto wawili alifichua kwamba Kelvin angepata pesa nzuri na hangemnunulia hata zawadi ndogo.

"Angeuza miwa apate kama elfu 40 na hata kukununulia hata slippers hawezi," alisema.

Kufuatia hayo, Cynthia alimtaka mumewe huyo wa zamani atafute mwanamke mwingine wa kuoa huku akiweka wazi kuwa hakuna uwezekano wa wao kurudiana.

"Nilikwambia tafuta mke uoe. Mahali nimefika siwezi kurudi nyuma tena. Kama ni kuoa nimekuruhusu. Tafuta mke uoe. Watoto wataishi. Mama ni mzima na watoto wako sawa," alisema.

Kelvin ambaye alisikika kushtuka alisema, "Wacha hasira itulie atarudi. Aliniambia wacha anyonye kidogo atarudi."

Cynthia hata hivyo alisisitiza kuwa hatarudi kwa ndoa hiyo," Tafuta mke uoe, sikurudii hata kidogo. Sitaki kukuharibia muda."

Je, una ushauri upi kwa wawili hao?