Patanisho: Jamaa alamikia mpenziwe kutopokea simu usiku, kukataa kurudi baada ya kwenda nyumbani

Collo aliibua malalamishi kuwa mke wake huwa hashiki simu zake mara nyingi anapompigia mida ya usiku.

Muhtasari

•Collo alisema ndoa yake ya chini ya mwaka mmoja ilianza kuyumba Disemba baada ya mkewe kwenda nyumbani na kukosa kurudi.

•Eliza alipopigiwa simu kwa mara ya pili, alibainisha kuwa hana shida na Collo na kueleza sababu zake kuenda nyumbani.

Image: RADIO JAMBO

Elikana Shikoli ,30, almaarufu kama Collo alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mke wake Caroline Nyako 'Eliza' ,32, ambaye alikosana naye mwishoni mwa mwaka jana.

Collo alisema ndoa yake ya chini ya mwaka mmoja ilianza kuyumba mwezi Disemba baada ya mkewe kwenda nyumbani na kukosa kurudi.

"Nimekosana na huyo msichana. Alitoka nyumbani Disemba mwaka jana.Nilingojako arudi, nikangojako, ila hakurudi. Nikamuuliza akasema niache kumsumbua," Collo alisimulia.

Aliendelea, "Nilimtumia pesa ya kurudi. Alisema atapanga atarudi lakini hajarudi. Huwa anasema anaenda kuona watoto. Akienda anarudi na anaenda tena. Alisema watoto waende wakasomee kwao."

Collo pia aliibua malalamishi kuwa mke wake huwa hashiki simu zake mara nyingi anapompigia mida ya usiku.

"Nikimpigia usiku kuna wakati huwa anashika na wakati mwingine anakosa kushika, mchana huwa anashika. Nilimtumia nauli mara moja akakuja, alipokuja akaenda tena," alisema.

Pia alidai kuwa mkewe alidai kuwa na mimba, jambo ambalo alitaka kuthibitishiwa, "Aliniambia ako na mimba. Nataka nijue kama ni ukweli ama ni kunifunika macho tu."

Bi Eliza alipopigiwa simu, Collo alikabiliana naye kwa ukali hadi akakata simu

"Wewe kichwa yako ni mzuri?" Eliza alimuuliza mumewe kabla ya kukata simu.

Alipopigiwa simu kwa mara ya pili, alibainisha kuwa hana shida na Collo na kueleza sababu zake kuenda nyumbani.

"Mimi sina shida na yeye. Anafaa kuelewa huwa naenda kuona watoto na kurudi. Nilimwambia atume nauli yeye hataki. Sio mara mingi nimeenda nyumbani. Nilikuwa nimerudi nyumbani kupeleka watoto shule," Eliza alisema.

Collo alimjibu, "Mimi nilikuwa nataka akuje na wao huku tukae nao. Sio kila mara kuenda nyumbani. Akuje nao tutawapeleka shule huku."

Eliza hata hivyo alimjibu, "Haiwezekani watoto kuenda na mimi Busia, watasomea huku. Wakifunga shule watanitembelea. Hawa watoto wako na baba yao, huyo ndiye anafaa kuwasaidia. Yeye ndiye alitaka wasomee huku Busia."

Aliongeza, "Wewe mwenyewe ni Juakali huwezi wasomesha. Hapo unakosea. Kama nauli ya 500 pekee yake nilikwambia utume hutaki, watoto utasomesha aje?.Sasa nikuje na miguu kutoka Kakamega? Kama nauli yenyewe huwezi kutuma, karo ya shule ndiyo utaweza?.. Hana kazi, watoto watasoma aje? Pia mimi sina kazi.. Yeye alikuwa tu mpenzi, mpaka nishughulikie watoto kwanza, siko tayari."

Kuhusu madai ya mimba, Eliza alisema, "Hiyo anaongea tu."

Collo alisema, "Sasa macho imefunguka.Huwa natamani usiku nisikie sauti yake lakini hashiki simu."

Eliza alimwambia, "Wee tuma nauli tuongee... Anitumie nauli tutaongeleshana wawili kwa nyumba."

Collo alimalizia kwa kusema, "Mimi bado nakupenda ndio maana nakufuatilia."

Je, maoni yako ni yapi kuhusu Patanisho ya leo?