Yassin Juma apata corona gerezani, Ethiopia

Mwandishi wa habari Yassin Juma, ambaye alikuwa ameshikiliwa nchini Ethiopia tangu mwezi uliopita amepatwa  na virusi vya corona, wakili wake Kedir Bullo amesema

Juma alikuwa anatarajiwa kufikishwa mahakamani katika mji mkuu wa Addis Ababa, lakini alishindwa kwa sababu ya kuugua, aliongeza bwana Bullo.

Mahakama ilitoa amri ya kuachiwa kwake kwa dhamana wiki iliyopita lakini polisi wa Addis Ababa walisema bado wanafanya uchunguzi dhidi ya madai yake na hivyo kuendelea kumshikililia kizuizini.

Mwandishi huyo alikamatwa pamoja na waandishi wa habari wawili wa Ethiopia. Walikuwa wanashutumiwa kwa kufanya ghasia na kupanga mbinu za kumuua maafisa wa juu wa Ethiopia.

Waandishi wote watatu walipinga madai dhidi yao.