

Waandamanaji watatu walikimbizwa katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta baada ya kujeruhiwa kwenye maandamano yaliyoanza jijini Nairobi mnano Jumatano.
Maelfu ya waandamanaji walijitokeza barabarani nchini siku ya Jumatano kuadhimisha mwaka mmoja tangu watu walipovamia bunge wakati wa kilele cha maandamano dhidi ya serikali, licha ya hofu kuwa wangekumbana na magenge yaliyoungwa mkono na serikali pamoja na ukatili wa polisi.
Wanaharakati na familia za waathiriwa walitoa wito wa maandamano ya amani ili kuadhimisha mwaka mmoja tangu siku mbaya zaidi ya machafuko hayo ambapo bunge lilivamiwa.
Mapema siku ya Jumatano, polisi walifunga barabara kuu zinazoelekea katikati mwa jiji la Nairobi, huku majengo ya serikali yakizingirwa na waya za miiba.

Maelfu ya waandamanaji, wengi wao wakiwa vijana wa kiume, walikuwa wakipeperusha bendera za Kenya na mabango yaliyoonyesha picha za waandamanaji waliouawa mwaka jana, huku wakipiga kelele "Ruto must go!"
Mbali na kuadhimisha kumbukumbu hiyo, hasira pia zimechochewa na ukatili wa polisi, hasa baada ya mwalimu mmoja kuuawa akiwa rumande mapema mwezi huu baada ya kukamatwa kwa kumkosoa afisa mwandamizi.
Polisi walisema maandamano yanaruhusiwa alimradi yawe ya amani na bila silaha.
Hata hivyo, kundi la waandamanaji wa amani wiki iliyopita lilivamiwa na genge kubwa la wanaume waliokuwa wakipanda pikipiki, wanaojulikana kama "goons", waliokuwa na mijeledi na marungu, wakionekana kushirikiana na polisi.
Ubalozi wa mataifa ya Magharibi nchini Kenya, ikiwemo Uingereza, Ujerumani na Marekani, ulilaani kwa taarifa ya pamoja matumizi ya wavuni walioajiriwa ili kuingilia au kuvuruga mikusanyiko ya amani.

Kuna chuki kubwa dhidi ya Ruto, ambaye alichaguliwa mwaka 2022 kwa ahadi ya kuleta maendeleo ya haraka ya kiuchumi.
Wengi wamevunjika moyo kutokana na hali ya kusuasua kiuchumi, ufisadi na ushuru wa juu, hata baada ya maandamano ya mwaka jana kumlazimu Ruto kufuta mswada wa fedha uliopingwa na wengi.
Serikali yake imejitahidi kuepuka kuongeza ushuru moja kwa moja mwaka huu.
Hata hivyo, kutoweka mara kwa mara kwa wakosoaji wa serikali kumewafanya wengi kumtuhumu Ruto kwa kuirejesha Kenya katika siku za giza za utawala wa kiimla wa miaka ya 1980 na 1990.
