"Tulipanga kupatana baada ya kutoka hospitali" Khaligraph afichua mazungumzo yake ya mwisho na Manduli
• Khaligraph amefichua kwamba alizungumza na marehemu kwa simu takriban miezi miwili iliyopita alipokuwa amelazwa hospitalini.
•Kwenye kibao 'Hao' kilichomfurahisha marehemu, Khaligraph amemtaja Orie Rogo Manduli kama mtu aliyejiamini.
Mwanamuziki mashuhuri wa nyimbo za kufoka Brian Ouko almaarufu kama Khaligraph Jones amemwomboleza mwanasiasa na mwanamitindo wa zamani marehemu Orie Rogo Manduli kwa ujumbe maalum.
Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Khaligraph amefichua kwamba alizungumza na marehemu kwa simu takriban miezi miwili iliyopita alipokuwa amelazwa hospitalini.
Msanii huyo ameeleza kuwa Manduli alimpigia simu kumuarifu kuwa alikuwa amependezwa na kibao chake 'Hao' ambacho ameshirikisha Masauti. Amesema kuwa hata walipanga kupatana ili washiriki mazungumzo wakati marehemu angepata nafuu na kutoka hospitalini.
"Takriban miezi miwili iliyopita nilipokea simu kutoka kwa marehemu Orie Rogo Manduli na akanieleza alivyokuwa amependezwa na kibao 'Hao'. Hata tulipanga kupatana tuzungumze baada yake kupatiwa ruhusa wa kuenda nyumbani kutoka hospitalini lakini Mungu alikuwa na mipango mingine" Khaligraph alieleza.
Hata hivyo mpango wao haukutimia kwani dereva huyo wa Safari Rally alipoteza maisha yake siku ya Jumatano akiwa nyumbani kwake jijini Nairobi. Marehemu alikuwa na umri wa miaka 73.
"Pumzika kwa amani, tupatane upande huo mwingine" Khaligraph alimwomboleza Manduli.
Kwenye kibao 'Hao' kilichomfurahisha marehemu, Khaligraph amemtaja Orie Rogo Manduli kama mtu aliyejiamini.
The video could not be loaded.
"Kukuwa celebrity kuwa ready for drama. Omba God akubless na self-esteem ya Pastor Ng'ang'a, na confidence ya Orie Rogo Manduli, na will power ya John Pombe Magufuli. Hata kama wengi watasema ni kiburi but that's the only way utaweza na hao mabully" Khaligraph amesema kwenye wimbo huo.