In Summary

•Mama Baha alitangaza habari za kuzaliwa kwa mwanawe siku ya Jumanne kupitia mitandao ya kijamii.

•Aliwahi kusema amekuwa akisubiria sana kuwa mzazi kwa kuwa katika maisha yake yote ameishi kupenda watoto.

Wanjiku Mburu almaarufu kama Mama Baha
Image: ELIZABETH NGIGI

Mwigizaji Wanjiku Mburu almaarufu Mama Baha kutokana na kipindi Machachari amebarikiwa na mtoto wake wa kwanza. 

Mama Baha alitangaza habari za kuzaliwa kwa mwanawe siku ya Jumanne kupitia mitandao ya kijamii.

"Burning Spear Jr" Wanjiku aliandika chini ya picha yake akimkumbatia mwanawe.

Baraka ya mtoto inakuja baada ya mwigizaji huyo kusubiri hatua ya kuwa na familia kwa miaka mingi.

Takriban miezi miwili iliyopita, Wanjiku alikiri kuwa alishangaa sana wakati alipofahamu kwamba ni mjamzito kwani ni jambo ambalo hakutarajia.

"Mwaka wa 2018  nilienda kuombea maisha yangu. Nilitaka kuombea mwelekeo wa maisha yangu. Kitu kimoja ambacho niliombea ni familia. Baada ya kuomba na kujifunga Mungu aliniahidi kunipa watoto. Nilicheka tu. Niliamua kusubiri. 2018, 2019 hata mtu sikupata sembuse watoto. Niliacha tu" Wanjiku alisema akiwa kwenye mahojiano na Mpasho.

Alisema mwanzoni alitilia shaka ujauzito wake na wakati tumbo lake lilipoanza kutokeza ndipo aliamini kuwa kuna kiumbe kilichokuwa kinajiumba ndani yake.

Wanjiku alisema amekuwa akisubiria sana kuwa mzazi kwa kuwa katika maisha yake yote ameishi kupenda watoto.

"Ni kitu ambacho niliishi kutaka. Hata hivyo nilikuwa nimesema iwapo nitakosa itakuwa sawa tu. Naamini kuwa Mungu hujibu maombi" Wanjiku alisema.

Maelfu ya Wakenya wameendelea kumpongeza mwigizaji huyo na kumtakia kila la kheri kwa baraka iliyomfikia.

View Comments