In Summary

• Okari amefunguka kuhusu mawazo ya kutaka kujidhuru ambayo yalimsumbua kufuatia talaka yake na mwanahabari mwenzake Betty Kyallo.

•Okari alisema alihangaika sana kuhusu jinsi angekabiliana na jamaa zake baada ya kuvunjika kwa ndoa yake miezi michache tu baada ya harusi. 

Dennis Okari na Betty Kyallo mnamo siku ya harusi yao.
Image: HISANI

Aliyekuwa mtangazaji wa habari wa NTV, Dennis Okari amefunguka kuhusu mawazo ya kutaka kujidhuru ambayo yalimsumbua kufuatia talaka yake na mwanahabari mwenzake Betty Kyallo.

Akiongea katika Kanisa la Jubilee Christian Church wikendi, Okari alikiri kwamba talaka yake na mama huyo wa bintiye ambayo ilikuja miezi michache tu baada ya harusi yao ya kifahari ilimuathiri sana.

Mwanahabari huyo mzoefu wa uchunguzi alifichua kwamba wakati fulani alifikiria kufanya ajali na gari lake ili kupoteza fahamu na kusahau masaibu yake.

"Nilikuwa nikiendesha gari kwenye Mombasa Road na nilifikiria kusababisha ajali na gari langu ili niende kwenye koma, na wakati nikiamka, yote hayo yawe yamepita. Nilitafuta jiwe lililokuwa barabarani lakini sikuweza kuliona usiku huo,” Okari alisimulia.

Alisema, "Kamwe hufungi ndoa ili kutaliki."

Okari alisema alihangaika sana kuhusu jinsi angekabiliana na jamaa zake baada ya kuvunjika kwa ndoa yake miezi michache tu baada ya harusi. Alikiri kwamba aliogopa kuonekana kama mtu aliyevunjikiwa na ndoa na hakujua jinsi ya kuvumilia.

Okari alikiri kwamba ilimchukua muda mrefu kukabiliana na unyanyapaa uliofuata talaka hiyo na kusema ilikuwa ngumu wakati aliingiliwa kanisani.

"Nilijipata mahali ambapo ndugu wenzangu waliniambia, 'Dennis, huwezi kutumikia kanisa kwa kiwango fulani wakati wewe ni mtaliki'," Okari alisema.

Mwanahabari huyo wa zamani wa NTV alisema alipata ugumu kumwamini mwanamke mwingine baada ya ndoa yake kuvunjila na akafichua kwamba ilimchukua takriban miaka mitatu kukabiliana na chuki na mchakato wa talaka.

Hata hivyo, baadaye aliweza kupenda tena na kukutana na mkewe Naomi ambaye ni mke wake wa sasa na mzazi mwenzake.

Dennis Okari na Betty Kyallo walichumbiana kwa takriban miaka minne kabla ya kufunga ndoa katika harusi ya kupendeza mnamo Oktoba 2, 2015 katika bustani la Marula Manor, mtaa wa Karen, jijini Nairobi. Kwa bahati mbaya, wanahabari hao wawili waliamua kutengana na kwenda njia tofauti takriban miezi sita tu baadaye na kuwaacha Wakenya wengi katika mshtuko mkubwa.

Wakati walipokuwa pamoja, wawili hao walibarikiwa na binti mzuri pamoja, Ivanna ambaye sasa wanashirikiana kumlea.

View Comments