In Summary

•Familia ya Blak Aende, ambaye ni baba wa marehemu ilitoa shukrani zao kwa sapoti ambayo wamepokea katika nyakati hizi ngumu.

•Ibada ya ukumbusho itafanyika katika kanisa la CITAM, mtaa wa Embakasi, jijini Nairobi kuanzia saa nne asubuhi.

Blak Aende na Nyaboke Moraa wamemuomboleza binti yao Marie Achieng

Familia ya marehemu Marrie Achieng imefichua mipango ya mazishi ya binti yao.

Katika programu iliyosasishwa iliyotolewa Jumatano mchana, familia ya Blak Aende, ambaye ni baba wa marehemu ilitoa shukrani zao kwa sapoti ambayo wamepokea katika nyakati hizi ngumu.

“Kwa niaba ya familia ya Dk. Blak, tunawashukuru kwa sapoti yenu inayoendelea. Familia imetulia kwa mipangilio ifuatayo ya matukio,” ilisoma programu iliyotolewa kwa niaba ya Blak Aende, babake marehemu Achieng.

Kulingana na programu hiyo, mkutano wa maandalizi utafanyika katika Mkahawa wa Che’C, ulio Green Park Terminus, jijini Nairobi mnamo Agosti 1, kuanzia saa kumi na moja jioni.

Mnamo Agosti 7, ibada ya ukumbusho itafanyika katika kanisa la CITAM, mtaa wa Embakasi, jijini Nairobi kuanzia saa nne asubuhi.

Hafla ya kuchangisha pesa itafanyika katika Mkahawa wa Chel'C siku ya Jumatano, Agosti 7, kuanzia saa kumi na moja jioni siku hiyo hiyo.

Mwili wa marehemu utaondoka Nairobi kuelekea Kisumu siku ya Ijumaa, Agosti 9, kabla ya maziko yatakayofanyika Jumamosi, Agosti 10. Atazikwa eneo la Kadongo, kaunti ya Kisumu.

Siku ya Jumanne, muigizaji Sandra Dacha, ambaye ni rafiki wa karibu wa mamake Marie, muigizaji Nyaboke Moraa, alitoa ombi la dhati kwa umma, akiomba usaidizi wa kifedha kumsaidia Nyaboke na mpenzi wake wa zamani kumpa binti yao mazishi ifaayo.

“Wapendwa, tujumuike pamoja kusaidia Gloria Anazidi Kuiva Moraa na Aende Blak kumpa binti yao mazishi yafaayo. Tunaomba msaada wako wa kifedha ili kufanikisha sherehe. Marrie atazikwa Jumamosi, Agosti 10, 2024, eneo la Kadongo, Kaunti ya Kisumu. Tafadhali tuma usaidizi wako kwa: PAYBILL No: 8023781, ACCOUNT No: Jina lako,” Sandra aliandika kwenye mtandao wa Facebook.

Marrie Achieng, ambaye alikuwa mzaliwa wa kwanza wa Nyaboke Moraa alipoteza maisha katika hali isiyojulikana mnamo Jumapili, Julai 28.

Siku ya Jumatatu, muigizaji huyo mahiri aliomboleza binti yake katika chapisho la kwanza la mtandao wa kijamii tangu kifo chake cha kusikitisha.

"Nitaanzia wapi?" Nyaboke Moraa alisema kupitia mtandao wa Facebook.

Pia alichapisha video ya kumbukumbu iliyomuonyesha akicheza dansi na marehemu binti yake na kuiambatanisha na emoji ya mapenzi.

Siku hiyo hiyo, mzazi mwenza wa Bi Moraa, mfanyabiashara Blak Aende pia aliomboleza kifo cha binti yao Marrie Achieng.

Blak Aende aliandika kumbukumbu fupi na ya kihisia kwa binti yake akisema kwamba Jumapili ilikuwa moja ya siku mbaya zaidi maishani mwake.

"Ni Siku ya giza. Siwezi kumhoji Mungu, ninamwachia kila kitu (Mungu)," Blakaende aliandika kwenye akaunti zake za mitandao ya kijamii.

Baadaye aliweka chapisho lingine likimuonyesha akiwa ndani ya ndege akisafiri nyumbani na juu yake akaandika, "Safari ya ndege ngumu zaidi kuchukua," ikisindikizwa na emojis za moyo mweusi.

View Comments