Sheikh.Mohammed.Al.Makhtoum

Mfalme wa Dubai, mmoja wa viongozi wakuu katika eneo la mashariki ya kati na mkewe aliyetoroka wameanza makabiliano ya mahakamani mjini London kuhusu wanao.

Mkewe Sheikh Mohammed Al Makhtoum Bintimfalme Haya Bint al-Hussein ni mtu wa tatu wa familia hiyo kutoroka ufalme huo wa UAE.

Mwezi huu aliripotiwa kuwa jijini London ambapo anajificha kwa kuhofia maisha yake.

Mahakama hiyo ya Uingereza inaangazia kuhusu watoto wao ambao alitoroka nao.

Bintimfalme Haya ambaye alizaliwa nchini Jordan na kusoma katika shule ya kibinfasi nchini Uingereza ni dada wa kambo wa mfalme wa Jordan King Abdullah wa pili.

Alifunga ndoa na Sheikh Makhtoum 2004, na kuwa mkewe wa sita na mdogo. Sheikh Makhtoum mwenye umri wa miaka 70 ana watoto 23 kupitia wake tofauti.

Bintimfalme Haya alitorokea nchini Ujerumani ili kujaribu kutafuta hifadhi , lakini ilibainika mwezi huu kwamba alikuwa akiishi mjini London hususan katika nyumba yenye thamani ya £85m iliopo bustani ya Kensington.

Inaaminika kwamba bintimfalme Haya atataka kusalia Uingereza.

Hatahivyo iwapo mumewe atataka arudi Dubai hatua hiyo inaweza kuwa hali ngumu ya kidiplomasia upande wa Uingereza ambayo mshirika mkuu wa UAE. Baada ya kutoroka , Sheikh Makhtoum aliandika shairi la kukasirika akimshutumu mwanamke huyo ka kumsaliti na kulichapisha katika mtandao wa Instagram.

Kwa nini Bintimfalme Haya alidaiwa kutoroka?

Duru karibu na bintimfalme huyo zilisema mapema mwezi huu kwamba aligundua ukweli kuhusu kurudi Dubai mwaka uliopita kwa Sheikha Latifa, mmoja wa watoto wa Sheikh Makthtoum.

Sheikha Latifa alitoroka UAE kupitia meli baada ya kupata msaada wa raia mmoja wa Ufaransa , lakini alipatikana na watu waliokuwa wamejihami katika pwani ya India. Baadaye alirudishwa Dubai.

Wakati huo, bintimfalme Haya aliitetea Dubai kuhusu kisa hicho , akidai kwamba Sheikha Latifa alitumiwa vibaya lakini kwamba alikuwa salama Dubai

Wanaharakati wa haki za kibinadamu wanasema kwamba alitekwa.

Hatahivyo Duru za baadaye zimedai kwamba Binti mfalme Haya alikuwa na habari zinazohusiana na kesi hiyo na kutokana na hilo alipokea shinikizo kali kutoka kwa familia ya mumewe.

-BBC

View Comments