- uhuru.plane.jfif
- Uhuru.Puttin.jfif
- Uhuru.plane.2.jfif

Rais Uhuru Kenyatta amefanya jumla ya ziara 31 za kimataifa tangu aapishwe kwa muhula wa pili miaka miwili iliyopita na kuibua maswali kuhusu manufaa ya safari zake.

Huku wizara ya fedha ikitangaza kutekeleza mikakati ya kupunguza matumizi ya pesa za serikali na kupunguza mgao wa pesa kwa idara mbali mbali, bajeti ya urais inayojumuisha Ikulu ya rais na afisi ya naibu rais William Ruto haijapunguziwa hata senti moja.

Katika muda wa miezi 14, rais ametua katika zaidi ya nchi 30 zikiwemo Urusi, Japan, Ethiopia, Rwanda, Uganda, Tanzania, Afrika Kusini, Sudan Kusini na Uingereza. Kwa sasa yuko nchini Saudi Arabia kwa ziara ya siku zisizojulikana kabla ya kuelekea nchini Botswana kuhudhuria kuapishwa kwa rais mteule Eric Mokgweetsi Masisi.

Katika muhula wake wa kwanza, rais Kenyatta alifanya jumla ya ziara 86 za kimataifa. Mwaka wa 2015 alifanya ziara nyingi zaidi kwa kuzuru jumla ya miji mikuu 26. Tangu achukuwe mamlaka ya kuongoza taifa, kinaya ni kwamba rais Kenyatta amekuwa akihimiza kupunguzwa kwa matumizi ya pesa za serikali na hata wakati mmoja akawambia wakenya kwamba yeye na naibu rais William Ruto watapunguzwa mshahara.

Safari nyingi za kimataifa za rais zimeibua mjadala mkali na kukashifiwa huku maswali yakiulizwa kuhusu faida ya safari hizo kwa taifa. Ikulu ya rais awali ilikuwa imetetea safari za Kenyatta kimataifa, ikidai kwamba nyingi ya safari hizo ni za kuvutia uwekezaji nchini.

Kulingana na ripoti ya mdhibiti wa bajeti ya kitaifa iliyowasilishwa bungeni, Kenyatta na naibu wake Ruto walikuwa wameongeza gharama zao za usafiri mara tano zaidi kufikia mwezi Machi mwaka huu.

Huku rais Kenyatta akipendelea kusafiri nje ya nchi, Ruto anapendelea kufanya ziara za humu nchini akihutubia mikutano ya hadhara. Kulingana na mdhibiti wa bajeti, idara ya urais ilitumia shilingi milioni 190 kwa kipindi cha miezi tisa pekee.

Ziara za kimataifa za Uhuru ni kinyume cha mtanguzili wake Mwai Kibaki ambaye alifanya jumla ya ziara 33 pekee kwa muda wa miaka 10 akiwa rais. Katika muhula wake wa kwanza Uhuru alivunja rekodi kwa jumla ya ziara 93 na kumfanya rais wa Kenya aliyefanya safari nyingi zaidi za kimataifa.

Babake, na mwanzilishi wa taifa la Kenya Jomo Kenyatta alikuwa muoga wa kutumia ndege na hakupenda kusafiri nje ya Kenya. Kwa wakati mmoja mwaka 2015, wakenya walimbandika Uhuru jina "Kenya's visiting President," kutokana na ziara zake za kila mara.

“Mbona twahitaji rais anayekodisha ndege za kibinafsi wakati makampuni nchini yanafungwa, vijana hawana ajira?,”Ndungu Wainaina, mkurugenzi wa kituo cha sera na utatuzi wa mizozo alisema.

Mwezi Septemba mwaka huu, wizara ya fedha ilitangaza mikakati mahsusi ya kupunguza bajeti ya serikali kutokana na upungufu wa jumla ya shilingi bilioni 91 katika makadirio ya bajeti ya kitaifa.

Kwa kawaida kafari ya rais ya nje ya nchi hujumuisha pia kitengo chake cha ulinzi, maafisa wa serikali na wasaidizi wake.

Katika ziara ya Urusi na Japan, Serikali ilikodisha ndege aina ya “Airbus A318 Elite”, ndege ya kifahari yenye uwezo kubeba abiria 19 na inayogharimu shilingi milioni 1.8 kila saa.

Uhuru alisafiri moja kwa moja kutoka Mombasa hadi Tokyo Japan baada ya kuongoza shereza za Mashujaa. Kisha alielekea Soshi Urusi na kurejea Nairobi Ijumaa iliyopita kusherehekea siku yake ya kuzaliwa.

Aliondoka tena siku ya Jumatatu kwenda Saudi Arabia na anatarajiwa kuelekea Botswana moja kwa moja kutoka Saudia Arabia.

View Comments