Serikali yaondoa sheria kali za kupambana na ufisadi
Serikali imeondoa bungeni sheria ambazo zingekabiliana kikamilifu na ufisadi na kufichua vita vya ndani kwa ndani miongoni mwa mashirika ya serikali ambayo yana jukumu la kupambana na ulaji rushwa.
Miswada hiyo ilikuwa imetegemewa pakubwa sana kuweza kupiga jeki vita dhidi ya ufisadi na ilikuwa imependekeza maafisa wote wa umma wanaoshtakiwa akiwemo naibu wa rais kuondoka afisini.
Hata hivyo imeibuka kwamba malumbano baina ya mashirika mbalimbali yamefanya miswada hiyo kuondolewa hasa baada ya shirika kutwaa mali iliyopatikana kwa njia za kifisadi ARA kulalamika vikali.
ARA ilikuwa imesema kwamba sheria hizo zingeyafanya mashirika mengine ya serikali kuchukua sehemu ya majukumu yake.
Siku ya Jumatano, spika wa bunge Justin Muturi alitangaza kwamba amekubali ombi la kiongozi wa wengi bungeni kuondoa marekebisho hayo katika sheria za kupambana na ufisadi.
Muturi, amesema katika ujumbe wake wa wabunge kwamba ni muhimu kutoa fursa kwa majadiliano zaidi kati ya mashirika mbalimbali ya serikali kabla ya marekebisho hayo kuwasilishwa tena bungeni .