In Summary

•Moto huo ambao chanzo chake bado hakijajulikana  uliteketeza Kanisa la Africa Divine na nyumba kumi na tatu jirani.

•Polisi wanachunguza chanzo cha moto uliozuka katika duka la dawa la Hospitali ya Pumwani Maternity.

Moto moto
Image: PICHA YA MAKTABA

Mali ya thamani ya mamilioni ya pesa iliharibiwa Ijumaa jioni baada ya moto kuzuka katika mji wa Limuru.

Moto huo ambao chanzo chake bado hakijajulikana kufikia wakati wa kuchapishwa kwa taarifa hii, uliteketeza Kanisa la Africa Divine na nyumba kumi na tatu jirani.

Hakukuwa na majeruhi walioripotiwa.

Naibu Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Limuru Paul Yator alisema moto huo ulizuka mwendo wa saa kumi na moja jioni.

"Tutawasaka waliojinufaisha na tukio hilo kupora mali ambayo wakaazi walikuwa wakijaribu kutoa kutoka kwa moto huo," aliongeza.

Yutor pia alisema wameanzisha uchunguzi kuhusu chanzo cha moto huo.

Wakati huo huo, polisi katika mtaa wa Buruburu, Nairobi, wanachunguza chanzo cha moto uliozuka katika duka la dawa la Hospitali ya Pumwani Maternity.

Moto huo unasemekana kuanza mwendo wa saa tisa unusu usiku wa Ijumaa lakini ukazimwa muda mfupi baadaye na kikosi cha zimamoto na uokoaji cha Kaunti ya Nairobi.

Hakukuwa na majeruhi.

"Kikosi cha zimamoto na uokoaji cha Kaunti ya Jiji la Nairobi kilijibu kwa dakika 10 na kuzima moto huo. Hakukuwa na majeruhi," CEC wa Afya wa Kaunti Anastacia Nyalita alisema.

View Comments