In Summary

•Inasemekana Mgunda ni miongoni mwa magonjwa yanayoambukizwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu na unasababishwa na Bakteria aina ya Leptospira interrogans.

Image: BBC

Serikali ya Tanzania imebaini kuwa ugonjwa unaoua watu kusini mwa Tanzania ni homa ya Mgunda.

Waziri wa Afya Mheshimiwa Ummy Mwalimu amewaambia waandishi wa habari kuwa upimaji wa sampuli za wagonjwa waliokuwa wakiugua katika Wilaya ya Ruangwa katika Mkoa wa Lindi umethibitisha mlipuko huu kuwa wa ugonjwa unaoitwa kitalaamu Leptospirosis, Field Fever au kwa lugha ya Kiswahili inajulikana kama Homa ya Mgunda.

Waziri Ummy amesema hayo leo mara baada ya kutembelea Wilaya ya Ruangwa katika Mkoa wa Lindi ambako kumezuka Mlipuko wa Ugonjwa huo na kuzungumza na Waandishi wa Habari.

Kwa mujibu wa Waziri Ummy Homa ya Mgunda ni miongoni mwa magonjwa yanayoambukizwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu na unasababishwa na Bakteria aina ya Leptospira interrogans.

"Ugonjwa huu umekuwepo katika maeneo ya kitropiki ambayo ni yenye hali ya joto katika mabara ya Amerika ya Kaskazini, Amerika ya Kusini, Afrika, Asia na Australia.,' amenukuliwa na kuongeza 'Wanyama aina za panya, kindi, mbweha, kulungu, swala, na wanyamapori wengine wameripotiwa kupata maambukizi ya vimelea hivi na kuwa chanzo cha maambukizi kwa binadamu" amesema.

Hadi kufikia siku ya tarehe 17 Julai 2022, kulikuwa na wagonjwa 20 na vifo vya watu watatu (3) vilivyotokana na ugonjwa huo. Kwa mujibu wa taarifa ya Waziri Ummy, kwa sasa, wagonjwa wawili pekee wenye dalili ndiyo bado wamelazwa katika eneo lililotengwa kwa ajili ya matibabu.

Vile vile, timu zimeendelea na ufuatiliaji wa watu waliotangamana na wagonjwa ambapo mpaka sasa, Serikali inasema hakuna aliyeonesha dalili za ugonjwa.

View Comments