In Summary

• Katika kilele cha janga la Covid, Rais wa Urusi Vladimir Putin alikuwa mmoja wa viongozi wa serikali waliolindwa zaidi ulimwenguni.

Image: BBC

Katika kilele cha janga la Covid, Rais wa Urusi Vladimir Putin alikuwa mmoja wa viongozi wa serikali waliolindwa zaidi ulimwenguni - bado hali iko hivyo, licha ya kulegezwa  kwa hatua za kupambana na  coronavirus kote ulimwenguni.

 Kila mtu aliye na ufikiaji ndani ya eneo la kilomita la kiongozi wa Urusi (na hiyo ni watu kadhaa, kama vile madaktari, wafanyikazi wa huduma, marubani na wengine wengi) lazima watumie wiki mbili katika karantini na kuchukua vipimo visivyo chini ya vinne vya Covid, na vile vile vingine. vipimo vya matibabu, ikiwa ni pamoja na katika baadhi ya visa  sampuli za kinyesi. Je, mfumo unaolinda afya ya Vladimir Putin unafanya kazi vipi?

“Na kisha ikawa zamu yangu.

Tulipeana mikono na nikampa salamu za heri [Vladimir Putin] kutoka kwa mashujaa wote wa vita katika jamhuri yetu," jenerali mstaafu kutoka eneo la Tatarstan la Urusi, Akhat Yulashev, aliambia vyombo vya habari vya ndani aliporejea nyumbani kutoka Moscow.

"Alitabasamu kwangu. Alifanya hisia kama hiyo!"

Mzee huyo mwenye umri wa miaka 94 alisafiri hadi Moscow kuhudhuria gwaride la Siku ya Ushindi ya Mei 9 katika eneo maarufu la Red Square. Lakini kwa sababu angemkaribia Bw Putin, ilimbidi kwanza akae kwa karantini kwa wiki mbili katika hoteli moja ya Moscow ambayo aliiita "ya kifahari"

'Matumizi yasiyo na kifani'

Image: BBC

BBC haikuweza kuzungumza na Jenerali Yulashev kibinafsi, lakini inafahamika kuwa alikuwa mmoja wa watu wapatao 400 waliowekwa karantini kwa wiki mbili katika hoteli za kifahari za Moscow (moja ya nyota tano na  nyingine ya nyota nne) kabla ya mkutano wa karibu na Kiongozi wa Urusi siku hiyo.

Inaonekana kwamba hata huku janga hilo likipungua na kutolewa kwa chanjo mbali mbali, hatua za kinga karibu na Bw Putin zimebaki kuwepo. 

Rais huzunguka makazi yake zaidi sasa kuliko hapo awali katika miaka miwili iliyopita, kama vile huduma yake na wafanyikazi wa matibabu - na kila mtu mwingine anayewasiliana naye.

Takwimu zinazopatikana wazi kutoka kwa vyanzo vya serikali ya Urusi zinaonyesha kuwa karibu rubles bilioni 3.2 ($ 54.6m) zilitumika kulinda afya ya Putin kupitia hatua hizi. Mikhail Fremderman, daktari wa Israel ambaye hadi 2014 alikuwa nchini Urusi, anaelezea kiwango chao kuwa hakijawahi kutokea. 

"Kutokana na hatua hizi, haiwezekani kuhukumu ikiwa rais wa Urusi anakabiliwa na matatizo makubwa ya kiafya. Kuna uwezekano mkubwa wa kuwa tahadhari za usalama."

Konstantin Balonov, daktari anayeishi Marekani ambaye amewatibu wagonjwa mahututi wa Covid, aliishi Urusi hadi katikati ya miaka ya 90. Anasema hatua hizo nyingi zinaweza kuhusishwa na madaktari wa Kremlin wanaokosea upande salama.

'Vipimo kupita kiasi'

Image: BBC

Wakati kulikuwa na kila sababu vipimo vya  Covid mapema kwenye janga hilo, kadiri wakati ulivyopita na idadi ya kesi nchini Urusi ilipungua, hatua hazikupungua. Licha ya ukweli kwamba Rais Putin aliripotiwa kupewa chanjo dhidi ya Covid, upimaji kwa kila mtu ambaye aliwasiliana naye ulibaki kuwa wa lazima.

Pia vipimo vipya viliongezwa, kama vile kupima kingamwili za Covid, mafua, baridi na maambukizi ya staph, pamoja na sampuli za kinyesi .

Kulingana na vyanzo vya wazi vya serikali, tangu mwanzo wa 2021, karibu watu 1,500 wamepitia upimaji wa kina.

Mnamo Februari 2022, baadhi ya vyombo vya habari vya Urusi vilivyotaja vyanzo visivyojulikana viliripoti kwamba baadhi ya wafanyakazi wa Kremlin waliokuwa na uwezo wa kumfikia rais walilazimika kuwasilisha sampuli za kupimwa mara moja kwa wiki.

Vyanzo wazi pia vinaonyesha kuwa wafanyakazi na  wanaohusika katika kumsafirisha rais wa Urusi pia hupimwa mara kwa mara. Kwa upande wao, ni aina mbalimbali za vipimo - kutoka kwa vipimo vya haraka vya PCR Covid hadi upimaji wa kingamwili hadi sampuli za kinyesi. Kwa jumla, wafanyakazi wa ndege wanaripotiwa kutumia $2.1m katika kipindi cha miaka miwili iliyopita kufanya vipimo . 

Mwezi Mei pekee mwaka huu, wafanyakazi wa ndege waliwasilisha    swabu 1,376 na sampuli 98 za kinyesi, pamoja na vipimo 447 vya damu. Idadi kubwa ilitumia wiki mbili katika karantini katika hoteli katika viunga  vya Moscow. 

Daktari mmoja wa Urusi, mtaalamu wa magonjwa ya kuambukiza, aliambia BBC kwamba "kiwango hiki cha kupita kiasi cha kupima" hakiwezi kuwa na madhumuni ya matibabu.

"Vipimo hivi vinaongeza vipimo vya kawaida vya PCR maradufu," anasema, akiongeza kuwa hajui njia ya kinyesi ya maambukizi ya Covid.

Kupima maambukizo mengine na kupunguza kasi ya kutangamana  na ulimwengu wa nje ni kawaida kwa wagonjwa mahututi, anasema daktari, lakini tu wakati wanakaribia kufanyiwa upasuaji.

Anasema kuna uwezekano kwamba vipimo  hivi vyote havitokani  na sayansi ya matibabu lakini badala yake ni jaribio la maafisa wa ngazi za chini "kujipendekeza kwa wakubwa wao - ili kuonyesha kwamba wamefikiria kila kitu."

Msafara wa matibabu

Image: BBC

Mnamo Machi 2021, Kremlin ilitangaza kwamba Rais Putin alikuwa amepewa chanjo. Baadaye ilitangazwa chanjo iliyotumika ilikuwa chanjo ya kwanza kutengezwa  nchini Urusi, Sputnik V. Michakato yake ya upimaji ilitiliwa shaka na wataalamu wengi nje ya Urusi.

Kufuatia chanjo hiyo, Vladimir Putin alirejea kusafiri mara kwa mara nchini kote, akikaa katika makazi yake nje ya Moscow. Katika safari hizi mara nyingi hufuatana na madaktari.

BBC imegundua kutoka vyanzo vya wazi kwamba hadi madaktari wanne huandamana na Rais Putin katika ziara yake ya kutembelea nyumba yake ya likizo kwenye Ziwa Uzhyn maridadi, takriban kilomita 400 kaskazini-magharibi mwa Moscow. Makumi ya maelfu ya dola zilitumika kwa malazi ya wafanyikazi wa matibabu. 

Pia kuna dalili za wazi kwamba madaktari huandamana na Vladimir Putin katika safari zake za kwenda kwenye makazi mengine, wakati huu huko Sochi kusini mwa Urusi.

BBC imegundua kuwa timu ya madaktari pia waliandamana na rais wa Urusi alipohudhuria vikao vya biashara huko St Petersburg na Vladivostok. Hili la mwisho ni kazi ngumu sana kwani Vladivostok iko Mashariki ya Mbali ya Urusi, safari ya saa 11 kwa ndege kutoka Moscow.

Vyombo vya habari huru vya Urusi vimeripoti kwamba baadhi ya wafanyikazi wa Kremlin wametumia hadi siku 150 kwa mwaka mmoja katika karantini katika vyumba vya hoteli pekee.

Je, hii inalinganishwaje na nchi nyingine?

Image: BBC

Daktari wa Israeli Mikhail Fremderman anasema kwamba hatua za sasa za Covid huko Israeli ni sawa kwa mkuu wa serikali kama zilivyo kwa raia wa kawaida. Hakuna hatua za ziada au vipimo vinavyoripotiwa  kufanyika hapo. Waziri Mkuu wa Israel anaandamana na madaktari, lakini kwa safari za nje tu.

Daktari wa Marekani Konstantin Balonov anasema hajawahi kusikia mtu yeyote akipimwa Covid kupitia sampuli za kinyesi na vipimo pekee anavyofahamu ni vipimo vya PCR au antijeni.

Balonov anasema vyanzo vyake vinavyofahamu itifaki za matibabu katika Ikulu ya White House vilithibitisha kwamba hakuna upimaji au karantini inayotumika kwa waandishi wa habari, ingawa mapema katika janga hilo, waandishi wa habari waliohudhuria mikutano ya waandishi wa habari katika Ikulu ya White walitakiwa kuwasilisha matokeo hasi ya mtihani wa Covid. na kuvaa kifuniko cha uso - hatua ambazo zilikuwa za kawaida katika maeneo yote ya umma nchini Marekani wakati huo.

View Comments