Joe Biden na Xi Jinping katika mawasiliano ya simu
Image: REUTERS

Katika mawasiliano ya simu yaliodumu kwa zaidi ya saa mbili , siku ya Alhamisi , rais wa Marekani na mwenzake wa China walirushiana cheche za maneno wakionyana kuhusu hali ya kisiwa cha Taiwan.

Rais wa Marekani Joe Biden alimwambia mwenzake wa China, Xi Jin Ping kwamba Marekani inapinga hatua yoyote ambayo inaweza kubadili hali iliopo katika eneo hilo ambapo Beijing inadai umiliki wake.

Biden alisema kwamba sera ya Marekani kuhusu kisiwa hicho inasalia , ikiunga mkono uhuru wake.

Beijing inakichukulia Kisiwa cha Taiwan kama kilichojitenga ambacho ni sharti kimilikiwe na taifa hilo na haijapinga uwezekano wa kutumia nguvu ili kuafikia malengo yake.

Kuhusu suala hilo, Xi aliitaka Marekani kuheshimu sera ya ‘China moja’, mbali na kumuonya kwamba anayecheza na moto ataungua’’.

Hali ya wasiwasi kuhusu suala hilo ilikuwa ikiongezeka tangu habari kwamba msemaji wa bunge la Marekani Nancy Pelosi angetembelea eneo hilo.

Hatahivyo wizara ya masuala ya kigeni ya Marekani imesema kwamba Pelosi hajatangaza ziara yoyote , lakini China imeonya kuhusu ‘hatua kali’ iwapo mwanasiasa huyo wa Democrat atafanya ziara hiyo.

Wiki iliyopita, Biden aliwaambia waandishi wa habari kwamba ujasusi wa kijeshi wa nchi yake "haufikirii kuwa ni wazo zuri" kwa ziara kama hiyo, lakini Ikulu ya White House ilisema matamshi ya Wachina "hayana maana na sio lazima."

Pelosi, ambaye ni wa tatu katika itifaki ya urais wa Marekani baada ya makamu wa rais, atakuwa mwanasiasa wa ngazi ya juu zaidi wa Marekani kusafiri hadi Taipei tangu 1997.

Spika wa Bunge la Marekani Nancy Pelosi alikuwa ametangaza kwamba atazuri taiwan mwezi April kabla ya kuahirisha safari hiyo baada ya kupatikana na virusi vya corona.
Image: GETTY IMAGES

Mkutano wa ana kwa ana

Biden na Xi pia walijadili kufanya mkutano unaowezekana wa ana kwa ana, afisa mkuu wa Washington alisema.

Biden alipokuwa makamu wa rais chini ya Barack Obama, alimkaribisha Xi wakati wa ziara ya kiongozi huyo wa China mwaka 2015, lakini hawajakutana ana kwa ana tangu 2015.

Ikulu ya White House ilisema viongozi hao wawili pia walijadili mada mbalimbali, ikiwa ni pamoja na mabadiliko ya hali ya hewa na usalama wa afya.

rais wa Marekani na mwenzake wa China walirushiana cheche za maneno
Image: GETTY IMAGES

Kwa muhtasari mfupi, Ikulu ya Marekani ilisema mazungumzo hayo ni sehemu ya juhudi za "kudhibiti tofauti kwa uwajibikaji" na kufanya kazi pamoja pale "maslahi yanapatana."

Katika taarifa ndefu, Beijing ilibaini kuwa masilahi yao mengi yalikuwa yanapatana.

Lakini alilaumu uhusiano unaozorota kwa Marekani, akikosoa mtazamo wa Washington wa kuichora China kama "mpinzani mkuu" na "mpinzani mkubwa wa muda mrefu."

Ni vigumu kuona chochote chanya. Na Rupert Wingfield-Hayes, mwandishi wa BBC kutoka Taipei

Mengi yanafanywa kutokana na ukweli kwamba Rais Xi alimwambia Rais Biden kwamba "yeyote anayecheza na moto ataungua."

Ni onyo kali kwa Marekani, lakini ambalo tayari halijawahi kutokea.

Wizara ya Mambo ya Nje ya China ilitumia lugha sawa kabisa wakati wajumbe wa Bunge la Marekani walipotembelea Taiwan mapema mwaka huu.

Maneno hayo hayo yalitumiwa na Wizara ya Ulinzi ya China katika onyo kwa Taiwan mwaka jana.

Ukweli kwamba sasa maneno hayo yametumiwa na Rais Xi sasa yana uzito zaidi.

Lakini hiyo haimaanishi kuwa China inatayarisha hatua za kijeshi dhidi ya Taiwan ikiwa, tuseme, Nancy Pelosi atawasili wiki ijayo. Badala yake, anaiambia Marekani kwamba ikiwa ataendelea na njia yake ya sasa, hatimaye kutakuwa na mzozo.

Ni vigumu kuona chochote chanya katika simu hii kuhusu uhusiano wa Marekani na China.

View Comments