Mume wa Maryam alimuomba amletee cheti cha ubikira maana hakutoka damu baada ya kufanya mapenzi
Image: BBC

Nchini Iran, ubikira kabla ya ndoa ni muhimu kwa wasichana wengi na familia zao. Wakati mwingine, wanaume huomba wathibitisha ubikira wao jambo ambalo Shirika la Afya Ulimwenguni linachukulia kama ukiukaji wa haki za binadamu. Lakini katika mwaka uliopita, idadi Wairani wanaotoa wito wa kukomeshwa kwa tabia hiyo kuongezeka.

"Ulinidanganya nikuoe kwa sababu wewe si bikra. Hakuna mtu ambaye angekuoa akijua ukweli."

Hivi ndivyo alivyosema mume wa Maryam walipofanya mapenzi kwa mara ya kwanza.

Alimhakikishia kwamba ingawa hakuwa anavuja damu, hakuwahi kufanya ngono hapo awali. Lakini licha ya uhakikisho wake, mume hakumwamini, na akamwomba atoe cheti ili kuthibitisha ubikira wake.

Sio kitu kipya Iran. Baada ya uchumba, wanawake wengi huenda kwa daktari wa kike kwa uchunguzi ili kuthibitisha kwamba hawajawahi kufanya ngono.

hata hivyo, vipimo vya ubikira havina thamani ya kisayansi, kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni.

Ushahidi wa Maryam unasema kwamba mlango wa uke wakw ni "unavutika", hivyo ina maana kwamba anaweza asitoe damu baada ya kufanya mapenzi.

"Utu wangu uliumizwa," anasema Maryam. "Sikufanya chochote kibaya, bado mume wangu alinitukana...sikuweza kuvumilia tena, hivyo nilichukua vidonge na kujaribu kujiua."

Kwa bahati nzuri Mariam alipelekwa hospitali kwa wakati na aliokolewa

Wito wa kukomesha tabia hiyo unaongezeka

Simulizi ya Maryam inaonyesha ukweli kwamba wanawake wengi wanaoishi Iran, Ubikira kabla ya ndoa bado ni muhimu kwa wasichana wengi na familia zao pia. Ni thamani iliyokita mizizi katika utamaduni wa jamii kubwa ya Iran.

Lakini kipindi cha hivi karibuni kulishuhudiwa baadhi ya viashiria vya mabadiliko. Wanawake na wanaume kutoka kote nchini wanafanya kampeni ya kukomesha upimaji bikira.

Novemba mwaka jana, watu 25,000 walitia saini ombi la mtandaoni ndani ya mwezi mmoja wakitaka kukomeshwa. Hii ilikuwa mara ya kwanza kwa idadi kubwa ya watu kupinga waziwazi vipimo vya ubikira nchini Iran.

"Ni uvamizi wa faragha, na ni matusi," anasema Neda. Neda ni mwanamke kutoka Tehran ambaye alipoteza ubikira wake alipofanya mapenzi na mpenzi wake alipokuwa mwanafunzi akiwa na umri wa miaka 17.

Anaongeza, "Niliogopa sana. Niliogopa kitakachotokea ikiwa familia yangu ingejua."

Kwa hivyo, Neda aliamua kutengenezea bikira.

Katika kufanya hivyo, upasuaji huo si kinyume na sheria lakini una madhara makubwa ya kijamii, hivyo hospitali hazikubali kuifanya.

Lakini Neda alipata kliniki ya kibinafsi ambayo ilikubali kufanya upasuaji kwa siri kwa kubwa.

“Nilitumia akiba yangu yote, na kuuza laptop yangu, simu yangu ya mkononi na dhahabu yangu,” anasema Neda.

Neda pia ilimbidi kutia sahihi hati yenye jmasharti iwapo kutatokea matatizo yoyote

Kisha mkunga akafanya upasuaji huo, ambao ulichukua kama dakika 40.

Lakini kupona kwa Neda kulichukua wiki kadhaa.

"Nilikuwa na uchungu mwingi," anasema. "Sikuweza kusogeza miguu yangu."

Neda aliwaficha wazazi wake.

"Nilijihisi mpweke sana. Lakini nadhani hofu yangu ni kwamba wangejua, ilinisaidia kustahimili maumivu."

Hata hivyo, mwisho mateso ambayo Neda aliyapata hayakuzingatiwa.

Mwaka mmoja baadaye, alikutana na mtu ambaye alitaka kumuoa. Lakini walipofanya ngono, hakutoka damu. upasuaji ulishindwa.

“Alinishtumu kwa kujaribu kumlaghai ili anioe,” asema Neda. “Alisema mimi ni mwongo, akaniacha.

Shinikizo kutoka kwa familia

Ijapokuwa Shirika la Afya Ulimwenguni linalaani vipimo vya ubikira kuwa ni kinyume cha maadili na kukosa uthibitisho wa kisayansi, tabia hiyo bado inafanywa katika nchi kadhaa, zikiwemo Indonesia, Iraq na Uturuki.

Shirika la Afya la Iran linashikilia msimamo wake kuwa hufanya vipimo hivi katika kesi maalum pekee kama vile kesi za kisheria au madai ya ubakaji.

Hata hivyo, maombi mengi ya vyeti vya ubikira bado yanatoka kwa wanaume na wanawake wanaopanga kufunga ndoa. Kwa hivyo, wanakimbilia kliniki za kibinafsi, kawaida huambatana na mama zao.

Vipimo hivi hufanywa na daktari wa uzazi au mkunga, ambaye hutoa cheti. Cheti hiki kina jina kamili la mwanamke, jina la baba yake, nambari yake ya kitambulisho na wakati mwingine picha binafsi. Ushuhuda unaeleza hali ya mlango wa uke na unasema, "Msichana huyu anaonekana kuwa bikira

Kwa familia za kihafidhina hati hiyo inasainiwa na mashahidi wawili kwa kawaida mama wa mchumba na mchumba.

Dk Fariba amekuwa akitoa vyeti hivi kwa miaka mingi. Anakiri kwamba ni tabia ya kufedhehesha, lakini anaamini kwamba inawasaidia wanawake wengi.

Wanawake hawa, anasema Fariba, "wako chini ya shinikizo kubwa kutoka kwa familia zao. Wakati mwingine, nalazimika kusema uwongo kwa wachumba. Ikiwa walifanya mapenzi pamoja na wanataka kuoana, ninasema mbele ya familia zao kwamba msichana ni bikira."

Kwa wanaume wengi, hata hivyo, kuoa bikira ni muhimu.

"Ikiwa msichana atapoteza ubikira wake kabla ya ndoa, hawezi kuaminiwa. Anaweza kumwacha mume wake kwa ajili ya mwanamume mwingine," anasema Ali, fundi umeme mwenye umri wa miaka 34 kutoka Shiraz.

Anaongeza kuwa amefanya mapenzi na wasichana 10: "nisingeweza kupinga."

Ali anakubali kwamba kuna undumilakuwili katika jamii ya Wairani, lakini haoni sababu ya kuacha mila.

"Kanuni za kijamii zinakubali kwamba wanaume wanafurahia uhuru zaidi kuliko wanawake," anaendelea.

Mtazamo wa Ali unashirikiwa na wengi, haswa katika maeneo ya vijijini ya kihafidhina ya Iran.

Licha ya kuongezeka kwa maandamano dhidi ya vipimo vya ubikira, ikizingatiwa kwamba wazo hilo limekita mizizi katika utamaduni wa Iran, wengi wanaamini kuwa serikali na bunge haziwezi kuweka marufuku yake hivi karibuni.

Matumaini ya siku zijazo

Baada ya miaka minne ya kujaribu kujiua na kuishi na mume mnyanyasaji, hatimaye Maryam aliweza kupata amri ya mahakama ya talaka wiki chache zilizopita.

"Itakuwa vigumu sana kumwamini mwanaume tena," Maryam anasema. "Sidhani kama nitaolewa katika siku za usoni."

Pamoja na makumi ya maelfu ya wanawake wengine, Maryam pia alitia saini mojawapo ya idadi inayoongezeka ya maombi yanayosambazwa mtandaoni kukomesha utoaji wa vyeti vya ubikira.

Ingawa hatarajii chochote kubadilika hivi karibuni, pengine si katika maisha yake, anaamini kuwa siku moja wanawake watakuwa na usawa zaidi na wanaume katika nchi yake.

"Nina hakika itatokea siku moja. Natumai kwamba hakuna msichana katika siku zijazo atakayepitia yale ambayo nimepitia."

Majina yote ya watu tuliozungumza nao yamebadilishwa ili kulinda utambulisho wao.

View Comments