In Summary
  • Hata hivyo, mapigano yaliendelea katika maeneo kadhaa ya Sudan, ikiwa ni pamoja na mji mkuu, Khartoum, ambapo RSF ilisema ngome yake imeshambuliwa.

Maafisa wa Sudan wanasema kuwa jeshi limesitisha mazungumzo ya kusitisha mapigano na wanamgambo wa Rapid Support Forces (RSF), wakilishutumu kundi hilo kwa kukiuka mara kwa mara makubaliano ya hapo awali ya kusitisha mapigano.

Jeshi lilichukua uamuzi huo "kwa sababu waasi hawajawahi kutekeleza hata moja ya vipengee vya usitishaji vita wa muda mfupi ambao ulihitaji kujiondoa katika hospitali na majengo ya makazi, na mara kwa mara wamekiuka makubaliano", afisa wa serikali, akizungumza kwa sharti la kutokujulikana, ameliambia shirika la habari la AFP.

Chanzo cha kidiplomasia cha Sudan pia kililifahamisha shirika la habari la Reuters kuhusu kujiondoa kwa jeshi katika mazungumzo tete ya kusitisha mapigano, ambayo yanalenga kuwezesha upatikanaji wa misaada ya kibinadamu.

Jeshi na RSF halijatoa maoni yao hadharani kuhusu hatua hiyo ya jeshi.

Siku ya Jumatatu, wapatanishi kutoka Marekani na Saudi Arabia walisema jeshi na RSF walikubaliana kuongeza muda wa usitishaji mapigano kwa ajili ya kutoa fursa ya msaada wa kibinadamu kwa siku tano.

Hata hivyo, mapigano yaliendelea katika maeneo kadhaa ya Sudan, ikiwa ni pamoja na mji mkuu, Khartoum, ambapo RSF ilisema ngome yake imeshambuliwa.

Jeshi lilisema kuwa limezuia shambulio la RSF kwenye mji wa kati wa El-Obeid.

 

 

 

 

 

 

View Comments