In Summary

• Mtu aliyewasiliana na mamlaka alikuwa amemkodisha marehemu, aliyejulikana kwa jina la Scott Jackson, kupeleka kuni nyumbani kwake wakati Omondi aliyekuwa uchi aliwashambulia.

Mwanaume aliyekamatwa
Image: Sagwe

Polisi huko Fort Worth, Texas nchini Marekani wanamshikilia kijana Mkenya mwenye umri wa miaka 27 ambaye anaripotiwa kumuua dereva wa lori la mizigo kwa kumpiga mara kwa mara na kuni kichwani.

Chrisantus Omondi alikamatwa usiku wa Januari 13, 2024 baada ya mkazi wa eneo hilo kuwafahamisha polisi kuhusu kuwepo kwa maiti katika ua wa mbele wa makazi yake kwenye Wendover Drive huko Fort Worth.

Mtu aliyewasiliana na mamlaka alikuwa amemkodisha marehemu, aliyejulikana kwa jina la Scott Jackson, kupeleka kuni nyumbani kwake wakati Omondi aliyekuwa uchi aliwashambulia wawili hao bila kutarajia, akidai kuwa walivamia eneo lake.

"Hii ni nyumba yangu, nina ufunguo hapa," Omondi alisema kama alivyonukuliwa na CBS.

Jackson na mwenye nyumba walimwagiza Omondi aondoke lakini inasemekana alichukua kipande cha kuni na kumpiga mhudumu huyo kichwani, na kumuangusha nje katika harakati hizo.

Kisha mshukiwa alielekeza mawazo yake kwa mwenye nyumba, na kumpiga kichwani na kumlazimisha mwanamume huyo kukimbilia nyumbani kwake kwa usalama.

Baadaye mwenye nyumba alipiga simu 911 na kuripoti tukio hilo. Akiwa kwenye simu na polisi, Omondi aliendeleza mashambulizi yake dhidi ya Scott, akimpiga kichwani mara kwa mara kabla ya kuelekea kwenye Airbnb ambayo inasemekana alikodi katika mtaa huo.

Polisi walipofika kwenye Airbnb, Omondi anasemekana kuwa hakushirikiana na kuwalazimisha maafisa hao kutumia bunduki ili kumdhibiti kabla ya kumzuilia na kumsafirisha hadi hospitali ya eneo hilo kufanyiwa uchunguzi.

Omondi anatazamiwa kushtakiwa kwa mauaji, shambulio la kikatili dhidi ya afisa wa usalama na kuzuia haki.

Bondi yake imewekwa kuwa USD 312,000 (takriban Ksh.50.4 milioni).

View Comments