GHASIA AFRIKA KUSINI
Uporaji Afrika Kusini: Tazama baadhi ya bidhaa za kushangaza ambazo raia wameonekana wakipora
Jamaa mmoja alishangaza wanamitandao baada yake kurekodiwa akipora geneza.
•Kwenye video moja, maafisa wa polisi walionekana wakipakia bidhaa ambazo walikuwa wameiba ndani ya gari la kazi. Ingawa haikuonekana wazi walikokuwa wanatoa bidhaa hizo, gari lao lilionekana kuwa karibu kujaa.
•Jamaa mwingine alirekodiwa akiwa amebeba mashine ya kutolea pesa (ATM). Haieleweki kwanini jamaa huyo akaamua kujisaidia na mashine hiyo ila huenda alidhani pesa huhifadhiwa hapo ndani.
Maafa, vurugu na uporaji vimeshamiri nchini Afrika Kusini kwa kipindi cha takriban wiki moja iliyopita. Hii ni baada ya aliyekuwa rais wa taifa hilo kukamatwa na kupewa kifungo cha miezi sita.
Wananchi ikiwemo maafisa wa polisi wameonekana wakipora mali kutoka maduka na mabiashara mbalimbali nchini humo.
Tukio moja la kuchekesha zaidi mwanaume mmoja alirekodiwa akiwa amebeba kipande kikubwa cha nyama kwenye mabega yake. Nyama aliyokuwa amepora mwanaume huyo ilionekana kuwa ya uzito wa zaidi ya kilo 50.
Kikundi kikubwa cha watu kilimfuata nyuma jamaa huyo huku kikicheka na kumpongeza kwa 'ushindi' wake.
Hilo sio tukio pekee ambapo polisi walionekana wakiiba. Inadaiwa kuwa maafisa nchini humo waliamua kujisaidia na bidha a za wizi kama raia wengine baada ya kushindwa kudhibiti hali.
Kwenye tukio lingine mwanaume mmoja alionekana akijaribu kusukuma televisheni kubwa ya ya upana wa inchi 58 kutoshea ndani ya gari ndogo. Hata hivyo televisheni hiyo ilikuwa kubwa zaidi haingetoshea kwenye mlango wa gari. Mwanaume huyo tayari alikuwa amejaza buti ya gari hilo na bidhaa zingine.