In Summary
  • Evelyn Joshua na mvutano wa uongozi ndani ya Kanisa alilolianzisha mumewe TB Joshua

Evelyn Joshua amekuwa kiongozi wa moja ya makanisa yenye ushawishi zaidi ya kiinjili, lakini mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 52 anakabiliwa na changamoto ya kuendeleza aliyoyaacha marehemu mumewe.

Kifo cha ghafla cha TB Joshua kilichotokea mwezi Juni akiwa na umri wa miaka 57 kiliibua mapambano ya kumrithi ambayo yamechukua miezi kadhaa kuyatatua.

Lakini malango makubwa ya kanisa lake la Synagogue Church of All Nations (SCOAN) katika mji mkuu wa Nigeria yamefunguliwa tena kuwapokea waumini kwa mara ya kwanza baada ya kufungwa kwa miezi mitano.

Alikuwa maarufu kwa unabii wake na kwa miujiza, iliyowavutia maelfu kutoka maeneo mbali mbali ya dunia kuja Lagos, wakiwemo wanasiasa kutoka Afrika na Amerika Kusini.

Kwa kawaida ni nadra kwa makabidhiano ya urithi wa uongozi wa kujadiliwa katika makanisa ya Nigerian ya Kipentekoste na mara kwa mara mjane wa marehemu hupewa mamlaka ya uongozi wa kanisa bila nafasi hiyo kupiganiwa.

Lakini katika SCOAN, Bi Joshua, ambaye ni Mchungaji aliyetawazwa, alikabiliwa na ushindani kwani hakuwa mjumbe wa bodi ya udhamini ya kanisa.

Hii ilichukuliwa na wapinzani wake kama ishara kwamba mume wake hakumfikiria kama mtu atakayemrithi.

Nabii na 'wanaume wake wenye busara'

Tofauti na wake wengine wa Wachungaji wa makanisa makubwa, Bi Evelyn, hakuonekana mara kwa mara kuwa mstari wa mbele katika shuguli za kanisa katika kipindi cha ndoa yao ya miongo mitatu.

TB Joshua, ambaye alifahamika na wajumbe wa kanisa lake la SCOAN kama "nabii", alifanya kazi na kikundi cha mitume aliowaita "wanaume wa busara" -ambao mmoja wao aliaminiwa kuandaliwa kumrithi.

Lakini baada ya kifo chake, wale wanaomtii Mke wa Joshua walichukua agizo la mahakama linalomfanya kuwa mjumbe wa bodi ya kanisa na hivyo kurahisisha njia yake ya kuchukua mamlaka.

Kanisa likamtangaza Bi Joshua kuwa kiongozi mpya wa Kanisa "chini ya muongozo wa Mungu", jambo lililofanya baadhi ya makundi ya watu wa kanisa hilo kutofurahishwa na ukosefu wa uwazi.

TB Joshua
Image: Twitter

Hasa wajumbe wa kikundi cha Global Congress cha SCOAN (GCSM), wakiungwa mkono na wajumbe wa ngazi ya juu wamehoji chaguo hilo.

Hatahivyo Bi Eveljyn aliondoa wasiwasi kwa yeyote mwenye swali juu ya nani anayedhibiti Kanisa hilo kwa kuongoza ibada ya kwanza ya kanisa la mumewe- SCOAN tarehe 7 Novemba tangu kifo cha mume wake.

Anaripotiwa kutopoteza muda wa kuonyesha mamlaka yake katika kanisa, akitumia miezi michache iliyopita kufanya baadhi ya mabadiliko ndani ya kanisa.

Video zimejitokeza za baadhi ya wafuasi wa kanisa, wengi wao raia wa kigeni ambao waliishi katika eneo la kanisa hilo kwa miaka mingi, wakihama, huku wakichekwa.

Mjumbe mmoja alielezea tukio hilo kama "ukaguzi".

Wale waliondoshwa kwenye eneo la kanisa walisemekana kuwa ni wapinzani wa uongozi wa Mke wa TB Joshua.

"Baada ya kifo cha mtume baadhi ya mitume wake hawakuongea na Evelyn kwa heshima na ukomavu ," Patrick Iwelunmor, msaidizi wa zamani wa masuala ya habari wa Joshuas, aliiambia BBC.

Kumekuwa na madai ya ufisadi na Shirika la kupambana na ufisadi la Nigeria , EFCC, liliithibitishia BBC kwamba linachunguza kesi ya wizi katika kanisa hilo.

Wajumbe wa uongozi wa ndani wa TB Joshua walishutumiwa kwa kutoweka na mifuko ya pesa taslim baada ya kifo chake.

Haijawa wazi ni nini kinachunguzwa, ingawa gazeti la Nigeria-The Punch liliripoti kwamba hiyo ilikuwa ndio sababu wajumbe wa Kanisa hilo wamejificha.

Pendekezo baaada ya tarehe ya kwanza

Bado kazi kubwa ya mke wa Joshua itakuwa ni kuwa na sifa ya kiroho kwa maelfu ya wafuasi waliomhusudu mume wake.

Walikuwa kwa haiba yake na uwezo wake aliojitangazia wa uponyaji na kwa hivyo hawatategemea lolote chini ya hilo kutoka kwa kiongozi mpya.

Gbenga Osinaike, mhariri mkuu wa gazeti la masuala ya kanisa nchini Nigeria- Church Times Nigeria, anakiri kwamba uteuzi wa mjane wa TB Joshua ulikuja kama jambo la kushtukiza.

"Alikuwa anahubiri mara kwa mara lakini TB Joshua hakuwahi kumtaja kama kiongozi ," aliambia BBC.

Lakini kwa mtu ambaye alipuuzwa kwa kiasi kikubwa, "akiwemo mume wake", Bi Joshua ameonyesha "nguvu yake ya ndani na uwezo wa kuliongoza Synagogue", anakiri.

Amekataa kurithi cheo cha mume wake cha "Msimamizi Mkuu", akisema kuwa bado mume wake ndiye mwenye mamlaka na kwamba "ameendeleza tu safari kuanzia pale alipoachia".

Na TB Joshua anaonekana katika kanisa, picha zake kubwa ziko katika kila kona ya jengo na mafundisho yake ya zamani yanatangazwa mara kwa mara kwenye vyombo vyake vya habari.

Mke wa Joshua pia anaonekana kurithi mtindo wake wa kuhubiri- akikatiza mahubiri kwa nyimbo za kuabudu mara kwa mara- sauti yake pia iliigiza ya marehemu mume wake katika ibada ya uzinduzi wa uongozi wake.

Joshua na mkewe kwa mara ya kwanza walikutana mwaka 1990 wakati alipomvutia kwa kuelezea hadithi ya maisha yake na kuandika jina lake kwenye kipande cha karatasi bila kusema neno lolote.

Walikaa dakika 45 pamoja walipokutana kwa mara ya kwanza, ambapo baada ya hapo alimuomba umuoe.

'Vipawa vya upatanishi'Bi Joshua ni pacha na ni mtoto wa kwanza kati ya watoto saba, akikulia eneo la Okala Okpuno katika jimbo Delta kusinini -mashariki mwa nchi ya Nigeria. Ingawa hakuanza kama mchungaji, alipata mafunzo na baadaye kutawazwa na mumewe kama mchungaji.

Mwaka 2009 alijielezea binafsi kama mtu mwenye vipaji vya kipekee katika kanisa la upatanishi - "mahusiano ya wazazi na watoto, ndoa na mambo kama hayo ".

Wachungaji wa makanisa makubwa nchini Nigeria mara kwa mara husema wana wito wa kibiblia-kama manabii Samuel na Paulo - wa kumtumikia Mungu.

Kulingana na TB Joshua, alisema alilalala siku tatu bila kuamka na kusikia sauti ikisema : "Mimi ni Mungu wako. Ninakupatia agizo la Kimungu la kwenda na kuendelea na kazi ya baba wa mbinguni."

Mke wa Joshua hajasema iwapo alipokea wito wa aina hiyo, lakini kwa baadhi ya washirika wake wa karibu wito wa mume wake unatosha.

"TB Joshua alikuwa nabii wa kuzaliwa, lakini mke wake amekuwa nabii kwa kuelekezwa. Mume na mke wamekuwa mwili mmoja, kwahiyo kwa umoja huo amempatia upako mke wake," alisema Bw Iwelunmo.

Ingawa baadhi ya wajane wa viongozi wa makanisa nchini Nigeria, kama vile Janet Onaolapo wa Abundant Life Gospel Mission na Margaret Idahosa wa kanisa la Church of God Mission International, wameweza kufanikiwa katika makanisa yao, hawa ni tofauti.

Makanisa mengi ya Kipentekoste nchini Nigeria yamejengwa kwa haiba za waasisi wake na mara nyingi huporomoka wanapofariki. Bw Osinaike anasema huenda hii ikawa pia hatma ya kanisa la TB Joshua-SCOAN.

"Inapokuja katika masuala ya kanisa watu wanatafuta suluhu, wanatafuta unabii, wanaangalia ni nani ameona maono yao," anasema.

"Hekalu [at SCOAN] bila shaka litaporomoka."

View Comments