In Summary

•Kamishna wa kaunti ya Kwale, Joseph Kanyiri alisema kuwa wazazi hao walikamatwa kutoka sehemu mbalimbali za kaunti hiyo baada ya kushindwa kueleza pahali watoto wao walipokuwa

•Elungata aliapa kuchukua hatua kali dhidi ya machifu iwapo watashindwa kuhakikisha kuwa watahiniwa wote wa KCPE 2020 wamejiunga na sekondari.

Baadhi ya wazazi ambao wallikamatwa katika eneo bunge la Kinango
Image: SHABAN OMAR

Habari na Shaban Omar

Wazazi 47 walikamatwa katika kaunti ya Kwale siku ya Jumatatu kwa kukosa kupeleka watoto wao shuleni.

Kamishna wa kaunti ya Kwale, Joseph Kanyiri alisema kuwa wazazi hao walikamatwa kutoka sehemu mbalimbali za kaunti hiyo baada ya kushindwa kueleza pahali watoto wao walipokuwa.

Eneo bunge la Kinango linaongoza kwa idadi ya watoto ambao hawakujiunga na kidato cha kwanza huku wazazi 18 kutoka huko wakikamatwa.

Operesheni hiyo ilifanywa na manaibu kamishna, machifu, wazee wa kijiji, polisi na  wakuu wa shule

Haya yalitokea siku moja tu baada ya kamishna wa eneo la Pwani John Elungata kulalamikia idadi ndogo ya wanafunzi ambao walijiunga na kidato cha kwanza katika eneo hilo.

Elungata aliapa kuchukua hatua kali dhidi ya machifu iwapo watashindwa kuhakikisha kuwa watahiniwa wote wa KCPE 2020 wamejiunga na sekondari.

Zaidi ya watahiniwa 22,000 walikalia mtihani wa KCPE 2020 katika kaunti hiyo.

Kaunti ya kwale imelegea katika kuhakikisha watoto ambao wamemaliza darasa la nane wamejiunga na kidato cha kwanza. Asilimia 69% pekee ya wanafunzi ambao walimaliza darasa la nane ndio wameweza kujiunga na kidato cha kwanza.

Kamishna Kanyiri alisema kuwa operesheni ile itaendelea siku ya Jumanne na kuagiza wazazi kushirkiana la sivyo wajipate gerezani kwa kukiuka sheria.

Wazazi ambao walikamatwa wanatarajiwa kufikishwa mahakamani leo (Jumanne)

View Comments